Na Joseph Lyimo, Simanjiro
WAVUVI
wanaofanya shughuli zao kwenye bwawa la Nyumba ya Mungu Wilayani
Simanjiro Mkoani Manyara, wametakiwa kufika kwenye vituo husika na
kupatiwa chanjo ya Covid-19 na kuachana na dhana potofu.
Wavuvi
hao wa Bwawa la Nyumba ya Mungu wametakiwa kupata chanjo hiyo kwani
hukutana na makundi ya wadau wa uvuvi wa samaki kutoka Wilaya tatu za
Simanjiro na Mwanga na Moshi za Mkoa wa Kilimanjaro.
Mmoja
kati ya wavuvi wa Kijiji cha Nyumba ya Mungu Kata ya Ngorika Joseph
Okoth amesema baadhi ya watu wamekuwa wanazusha dhana potofu ili watu
wasipatiwe chanjo.
Okoth
amesema baadhi yao wapotoshaji hao hawana elimu ya ugonjwa wa Corona
lakini wamekuwa mafundi wa kuzusha habari potofu ili hali hakuna faida
wanayoipata.
"Wewe huna
utaalamu wa afya wala hujui chochote juu ya virusi vya Corona lakini
unatoa elimu potofu juu chanjo ya Covid-19 utapata faida gani?" amehoji
Okoth.
Mvuvi mwingine
Davis Mosses amesema alichanja kwenye zahanati ya Kijiji cha Nyumba ya
Mungu hivyo anafanya shughuli zake bila hofu ya Corona.
Mosses
amesema baada ya kuona na kusikia kwenye vyombo vya habari namna watu
wanavyopata shida kwenye hospitali mbalimbali kwa kuvuta hewa kwa
kutumia mitungi alifika na kuchanjwa Agosti 5 mwaka huu.
"Pamoja
na mimi kuwa nimechanja bado navaa barakoa, natembea na kitakasa mikono
na kila nikifika eneo jingine nanawa na maji tiririka ili nisipate
maambukizi ya Covid-19 japokuwa nimeshapata chanjo," amesema.
Mfanyabiashara
wa samaki Mariam Hamis amesema wadau wa uvuvi wanapaswa kupata chanjo
hiyo kwani wanakutana na makundi mbalimbali ya watu tofauti hivyo
wanapaswa kujikinga.
Mariam
amesema wavuvi hao hukutana na wasafiri wanaosafirisha samaki maeneo
mbalimbali ya nchi hivyo chanjo ya Covid-19 itawasaidia kuliko kufanya
shughuli zao bila kuchanja.
"Wataalamu
wanasema ukichanja unaweza kupata Corona ila itakuja kwa heshima na
utapona tofauti na mtu asiyechanja hivyo tuchangamkie fursa hii,"
amesema.
Hata hivyo,
Diwani wa Kata ya Ngorika Albert Msole amewaasa wavuvi na wananchi wa
eneo hilo kuchangamkia fursa ya kupata chanjo kwani inapatikana.
Msole
amesema chanjo hiyo inapatikana kwenye zahanati iliyopo kwenye Kijiji
cha Nyumba ya Mungu, hivyo wananchi wa eneo hilo wajitokeze kupata
chanjo hiyo.
Amesema hivi
karibuni zahanati ya kijiji hicho ilipatiwa kiasi cha dozi 100 ya
chanjo hiyo ambapo hadi hivi sasa asilimia 70 ya chanjo hiyo
imeshatumika kwa watu kujitokeza na kuchanja.
“Wananchi
wa eneo hili hususani wavuvi waachane na habari potofu za kwenye
mitandao kuwa chanjo hiyo ina matatizo hivyo, wafuate ushauri wa
wataalamu kuwa chanjo haina madhara,” amesema Msole.
Mganga
mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Dkt Aristidy Raphael amesema chanjo ya
Covid-19 iliyopokelewa kwenye Wilaya hiyo ni dozi 1,000.
Dkt
Raphael amemaliza kwa kusema mwitikio wa watu kushiriki kwenye chanjo
hiyo siyo mbaya kwani watu zaidi ya 800 wameshajitokeza kuchanja hadi
hivi sasa.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...