Na Mwandishi Wetu, Ufaransa
UBALOZI wa Tanzania Paris Oktoba 10 mwaka 2021 umeshiriki katika jukwaa la lugha za dunia (Forum of Languages), lililofanyika katika viwanja vya Meya wa Jiji la Toulouse.
Jukwaa hilo, linaloandaliwa kila mwaka na taasisi ya Carrefour Culturel de langues, ilishirikisha mabanda 55 ambapo nchi na washiriki mbalimbali walikuwa wakionesha na kunadi lugha zao, mila, desturi na utamaduni.
Ubalozi wa Tanzania kwa kushirikiana na Chama cha Watanzania wa Ufaransa (CCWU) na kupitia kituo chao cha utamaduni na lugha (CCLT), uliamua kuchukua nafasi hiyo, kutangaza pia vivutio vyake vya utalii pamoja na kuvutia uwekezaji katika kutekeleza diplomasia ya uchumi.
Banda la Tanzania (pichani), lilitia fora kwa kutembelewa na wageni wengi zaidi ambao walipita kwenye banda hilo kuulizia masuala mbalimbali kama vile namna ya kujiunga na madarasa ya Kiswahili, kutembelea Tanzania Bara na Zanzibar, kufahamu historia ya Kiswahili, nanma ya kupata nafasi ya kufanya shughuli za kujitolea (Volunteering), kufanya biashara na uwekezaji.
Kwa upande wa utalii, machapisho na majarida yote yaliyopelekwa na Ubalozi yalichukuliwa na wakazi wa mji wa Toulouse katika maonyesho hayo ya siku nzima. Djillali Lahiani, Msaidizi wa masuala ya kijamii wa Meya wa Jiji la Toulouse aliusifu Ubalozi kwa kushiriki na kupongeza hatua zinazofanywa na Ubalozi kuitangaza lugha ya Kiswahili na utamaduni wake.
Lahiani alivutiwa pia na vivutio vya utalii alivyoviona kwenye majarida yaliyokuwepo na kusema atafikiria kutembelea Tanzania.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...