Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ndg. Daniel Chongolo amewaagiza Makatibu wa Wilaya maeneo yaliyobainika kuwa na kasoro ikiwemo baadhi ya watia nia kunyimwa fomu kwenye uchukuaji fomu ngazi ya shina nchi nzima kurudia zoezi hilo kwa sababu CCM sio Chama cha mtu binafsi bali cha wanachama wote.

Maagizo hayo ameyatoa leo Jumatano tarehe 20 Aprili, 2022 jijini Dar es Salaam alipokuwa kwenye Mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM ya Wilaya ya Ubungo na Kinondoni.

"Nawaagiza Makatibu wa wilaya, Ubungo na wilaya zote nchini, maeneo yote ambayo tumebaini yana changamoto ya watu kunyimwa kuchukua fomu za kugombea ndani ya chama, tunarudisha zoezi la kutoa  fomu, tunataka wale wote wenye dhamira ya kuchukua fomu wachukue bila kuwekewa vizuizi, hiki sio chama cha mtu, hiki sio chama cha maslahi binafsi, hiki chama ni cha wanachama, na ni lazima tutende haki kwa kuwa katiba yetu ya CCM inatutaka tufanye hivo." Katibu Mkuu Ndg. Chongolo ameeleza

Aidha ameoneza kuwa, "Dhamana tulizonazo hazijatupa haki ya kufanya maamuzi kwa ubinafsi, maeneo ambayo tumegundua yana hiyo changamoto napiga marufuku kuwanyima fomu wanachama, naagiza fomu ziendelee kutolewa kwa watu wote, zoezi la uchaguzi lisitishwe, wanachama wote wenye nia wapate haki ya kuchukua fomu na kugombea, kura ndizo zitakazo amua na sio vinginevyo", Katibu Mkuu Ndg. Chongolo amesisitiza

"Tunafuatilia na tukibaini kuna maeneo ambapo vitabu vilivyokuwa vimehakikiwa vimeongezwa majina ya watu wasiokuwemo kwenye utaratibu wa daftari la wanachama, Wakurugenzi /Makatibu wa uchaguzi watawajibika, hili sihitaji kusisitiza sana tutakutana baadae na hili ni kwa ngazi zote." Ameeleza Katibu Mkuu Ndg. Chongolo

Ameyataja baadhi ya maeneo yaliyobainika kuwa na changamoto hiyo kuwa ni pamoja na Wilaya ya Ubungo, Babati, Mbeya, Tabora na kusema ni lazima haki itendeke ndani ya chama kwa wanachama wote bila ubaguzi

Pia Katibu Mkuu amewaasa vijana kuacha kuwa wapambe tu wa wagombea, nao wana haki ya kugombea "Acheni kubaki vijana wa hamasa tu ama wapambe wa wagombea, chukueni fomu gombeeni na mkiona kuna mazingira ya kuwafungia milango, tuambieni haraka sisi tuna funguo za kufungulia."

Aidha Katibu Mkuu ameongeza kwa kuwapa Maelekezo Wenyeviti na Makatibu wa Umoja wa Vijana nchini Kukaa na vijana, kuwahamasisha kugombea na kusisitiza kuwa, hilo ni jukumu na wajibu usio na hiyari.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...