Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) amewataka askari wa uhifadhi nchini kujenga mahusiano mazuri na jamii inayozunguka maeneo ya hifadhi wanazozisimamia kwa kufanya kazi kwa kushirikiana nao katika masuala mbalimbali.
Ameyasema hayo leo Mkoani Kilimanjaro katika ziara ya kikazi alipotembelea Shamba la Miti la West Kilimanjaro kwa lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu na kusikiliza changamoto zinazowakabili Askari Uhifadhi kwa ili kuzipatia ufumbuzi.
“Jamii ikiwa haina mahusiano mazuri hata ninyi haya mashamba hamuwezi kuyaendeleza vizuri, kwa hiyo lazima muhakikishe mnajenga mahusiano mazuri”. Mhe. Masanja amesisitiza.
Amesema kuwa jamii inapokuwa hairidhishwi na utendaji kazi wa wahifadhi kunakuwa na migongano kati ya wananchi na wahifadhi hao na kupelekea wahifadhi kuchukiwa na wananchi.
Mhe. Masanja amewapongeza Askari Uhifadhi wa Shamba la Miti la West Kilimanjaro kwa kuendeleza mahusiano mazuri na jamii kwa kugawa miche, kutoa ajira na kugawa magogo ya kutengeneza samani.
Kuhusu changamoto ya moto katika mashamba, Mhe. Masanja ameelekeza wahifadhi kwenye mashamba yote nchini kushirikiana na Serikali za Mitaaa ili wananchi wanapoanza kuandaa mashamba yao wapate taarifa mapema na kuwaelekeza namna bora ya kudhibiti moto kwa lengo la kuukinga usisambae kuepuka hasara inayotokana na moto.
Aidha, amewataka wahifadhi wanaozunguka mlima Kilimanjaro kupanda miti kuzunguka mlima huo na kuhakikisha wanagawa miche ya miti kwa wananchi ili kuuzuia mlima usiendelee kuyeyuka.
Kwa upande wake Mhifadhi Mkuu Shamba la Miti West Kilimanjaro, Masawanga Ismail amesema kuwa shamba limeendelea kuwa na uhusiano mzuri na vijiji  na taasisi zinazolizunguka ambapo imekuwa msaada mkubwa hasa wakati wa matukio ya moto, upandaji wa miti na uhalifu ndani ya msitu.
Ameongeza kuwa shamba limekuwa likitoa mashamba ya kulima mazao ya chakula kwa jamii katika maeneo yanayovunwa miti kwa ajili ya maandalizi ya mashamba mapya ambapo kwa mwaka wa fedha wa 2021/2022 limetoa ploti zisizopungua 640.
Pia, amesema shamba limekuwa likitoa misaada mbalimbali kwa jamii inayolizunguka kama usafiri kwa wagonjwa, wafiwa na taasisi mbalimbali na  kugawa miche ya miti takribani laki moja na elfu kumi na tano katika mwaka wa fedha 2021/2022 na kutoa elimu ya ufugaji nyuki kwa vikundi vitano ambavyo vina wajumbe 95 vyenye jumla ya mizinga 250 ambavyo kwa mwaka huu vimezalisha asali kilo 200.
Kuhusu suala la utalii, Bw. Ismail amesema kuwa shamba hilo kwa mwaka huu limepokea watalii elfu 40 ambao wameingizia Serikali Dola za Kimarekani 70,335 na fedha za kitanzania takriban milioni 103.6.
Amesema mapato hayo yanatokana na vivutio vya utalii  vilivyomo kwenye shamba hilo kama mapango ya Grumeti na Mikingamo, Maporomoko ya Maji ,Bwawa la Kuogelea, Wanyamapori kama tembo na nyati, mito na  manthari nzuri.
Shamba la Miti West Kilimanjaro lilianzishwa mwaka ni 1940 kwa tangazo 227 chini ya sheria ya kikoloni kwa lengo la kuongeza uhifadhi wa vyanzo vya maji na kupunguza tatizo la mmomonyoko wa ardhi katika miinuko inayozunguka Mlima Kilimanjaro.




Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...