

*‘Njooni mjue bandari yenu inavyofanya kazi’
Na Chalila Kibuda, Michuzi Tv Mbeya
MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), imesema makontena yenye friji yanayofaa kwa kusafirishia bidhaa zinazoharibika mapema yapo lukuki tofauti Watanzania wanavyodanganywa na bandari shindani.
Mamlaka hiyo pia imewataka wakazi wa Mbeya kutembelea banda lao ili kujifunza namna bandari hiyo inavyofanya kazi.
Hayo yalisemwa na Ofisa wa Bandari (Utekelezaji), Denis Mapunda katika Viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya kwenye maonesho ya wakulima na wafugaji maarufu Nanenane.
Alisema mmoja wa wafanyabiashara wa matunda aliyewatembea bandani kwao alikuwa anatumia gharama kubwa kusafirisha bidhaa zake kutumia bandari ya nchi ya jirani.
Alisema mfanyabiashara huyo alikuwa anaambiwa kwamba bandari za Tanzania hazina kontena zenye friji maalumu wakati zimejaa tele.
Mapunda alisema bandari ni mali ya Watanzania na hivyo wana umuhimu wa kuitembelea banda lao ili kujua inavyofanya kazi.
“Mtu akitembelea hapa atajifunza mengi. Atajua namna tulivyoboresha bandari zetu, atajua namna tunavyofanya kazi, namna ya kusafirisha mizigo, kupokea na mengine mengi,” alisema.
Mapunda alisema katika maonesho hayo wameleta kila kitu cha mfano kuanzia meli za mizigo, kreni na vifaa vya ulinzi.
“Halikadhalika tumeleta hapa chuo cha bandari na namna ambavyo vijana wanaweza kujiunga nacho na kupata ujuzi mbalimbali,” alisema.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...