*Dkt.Komba adai fedha za kiinua mgongo hazina laana
Na Chalila Kibuda, Michuzi Tv
Watalaamu toka Chuo Kikuu Mzumbe waendesha mafunzo kwa wafanyakazi wanaotarajia kustaafu toka taasisi za umma kwa kuwajengea uwezo wa kutambua mbinu mbali mbali za uwekezaji na mipango ya fedha.
Akizungumza na washiriki wa mafunzo ya mipango ya kustaafu, kaimu Rasi wa Chuo Kikuu Mzumbe Ndaki ya Dar es Salaam, Dkt Coretha Komba, amesema kuwa wastaafu wengi hasa wa zamani walikuwa hawana utaratibu wa kupewa mafunzo na matokeo yake fedha walizokuwa wakizipata walikuwa wakizifanyia visivyo na kusema fedha za kustaafu zina laana kumbe laana hiyo imetokana na kutokua na mafunzo ya kitaalaam ya kutumia fedha hizo.
Dkt. Komba azitaka taasisi za Serikali na Sekta binafsi kuleta watumishi Chuo Kikuu Mzumbe ili kujengewa uwezo wa uelewa wa mbinu mbalimbali za uwekezaji na mipango ya fedha.
Mratibu wa Mafunzo hayo toka Chuo Kikuu Mzumbe Ndaki Dkt. Daudi Pascal Ndaki amesema kuwa mafunzo ya namna hii ni muhimu kwa watumishi kwani uelewa wa mbinu za uwekezaji na mipango ya fedha kabla ya kustaafu hutoa nafasi ya kujiandaa mapema na kuyafanya maisha ya kustaafu kuwa ya raha na mustarehe kwa sababu ya uhakika wa kumudu gharama za maisha kutokana na uwekezaji sahihi na mipango ya fedha inayoendana na kiwango cha kiinua mgongo.
Dkt.Ndaki amesema kuwa Chuo Kikuu Mzumbe kimekuwa kikitoa mafunzo ya namna ya kujiandaa na kustaafu kwa watumishi mara kwa mara. Katika mafunzo yaliyowahi fanyika na haya yanayoendelea watumishi hufundishwa kwa vitendo elimu ya mipango binafsi ya fedha na uwekezaji katika soko la mitaji na dhamana ikiwemo hati fungani, uwekezaji wa vipande na maeneo mengine ambapo ni kazi kuchagua tu.
Kwa upande wa mstaafu mtarajiwa, Mkurugenzi wa Kitengo cha Manunuzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira jiji la Arusha Ndugu Charles Kondela amesema kuwa mafunzo hayo ni muhimu sana kwao katika kuwajengea uelewa wa namna ya kuwekeza fedha za kiinua mgongo lakini pia kuelewa mipango sahihi ya fedha na maana halisi ya maisha baada ya kustaafu.
Ndugu Kondela anakishukuru sana Chuo Kikuu Mzumbe kuandaa mafunzo ya kuwaandaa watumishi na mbinu mbali mbali za uwekezaji, mipango ya fedha na uelewa wa maisha baada ya kustaafu. Ndugu Kondela aliendelea kusisitiza kuwa Chuo Kikuu Mzumbe ni mkombozi kwa Wastaafu watarajiwa kwani mafunzo yao yamesheheni kujifunza kwa vitendo.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...