Na Khadija Kalili 
TAASISI ya Kuzuia na  Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Pwani  itawachukulia hatua baadhi ya watu wanaosimamia miradi ya maendeleo ambayo imeonekana kuwa na mapungufu na kuisababishia serikali kukosa mapato.
Yamesemwa hayo leo  Novemba 15, 2022  na  Kamanda wa TAKUKURU Mkoa wa Pwani Christopher Myava alipozingumza na Waandishi wa Habari Ofisini kwake Kibaha mkoani Pwani amesema taarifa  hii ni kwa mujibu wa ripoti ya kipindi cha  robo mwaka Julai  hadi Septemba  mwaka huu, amesema kuwa  Takukuru imefuatilia miradi 26 yenye thamani ya shilingi Bil. 5.7 na kuikuta baadhi ikiwa na mapungufu.
Kamanda Myava amesema kuwa kuwa uchunguzi unaendelea kwenye miradi hiyo na wahusika wakibainika watachukuliwa hatua kali kwa mujibu wa sheria.
Ameitaja baadhi ya  miradi iliyofuatiliwa  kuwa ni kwenye sekta za Elimu, Afya, Maji, Barabara, Ardhi na Maendeleo ya jamii.
Aidha ameweka wazi kuwa  mikakati waliyojiwekea  TAKUKURU  katika kipindi cha miezi mitatu ijayo kuwa ni kufanya ufuatiliaji na uchambuzi wa mifumo ili kuziba mianya ya rushwa itakayobainika.
Kamanda Myava amesema kuwa bila rushwa maendeleo yatapatikana na huduma za jamii zitakuwa bora na zitapatikana kirahisi na kupunguza kero kwa wananchi.
Amesema kuwa kwa  kushirikiana na  vyombo  vingine  vya Ulinzi na Usalama  imebainika uwepo wa vifaa  vya ujenzi  visivyo  na ubora  katika ujenzi  wa shule  ya sekondari  mpya Jibondo iliyopo Wilayani Mafia, ambapo matofali 6,000 hayakukidhi viwango  baada ya upimaji  wa kitaalam  kufanyika hivyo mzabuni aliagizwa  kutoyatumia na kunyang'anywa  kazi hiyo  na akapewa mzabuni Mwingine.
Aidha Kamanda Myava amesema kuwa jumla ya malalamiko 98 yaliyopokelewa  kati ya  hayo 42 yalihusu  rushwa na majalada mapya  ya uchunguzi  yamefunguliwa na uchunguzi ukikamilika  hatua kali  za kisheria zitachukuliwa. Malalamiko 56  hayakuhusu  rushwa, katika malalamiko  hayo  yasiyohusu rushwa 25 walalamikaji  walishauriwa, malalamiko 11 yalihamishiwa taasisi nyingine na malalamiko 20 yalifungwa baada ya walalamikaji kupata  suluhu ya malalamiko yao.
Aidha mashauri mengine 13 mapya  yalifunguliwa  Mahakamani hivyo kufanya mashauri 29  kuendelea  Mahakamani  na hakuna shauri lililoamriwa. Amewashukuru  wanchi wa Mkoa wa Pwani  huku akiwataka kuendelea  kuunga mkono juhudi  za Taasisi hiyo  katika mapambano dhidi ya rushwa.
"Nawasihi wananchi wa Pwani kuendelea   kusimamia miradi  ya maendeleo  inayoendelea katika  maeneo  yenu  ili kuzuia  vitendo viovu vya  rushwa katika utekelezaji  wa miradi hiyo  na kwa wale wanaoendekeza  vitendo  vya rushwa  ninawaambia TAKUKURU  Mkoa wa Pwani haina uvumilivu  kwa wala rushwa hivyo basi tushirikiane katika kutokomeza vitendo vya rushwa" amesema Kamanda Myava.
Kamanda Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Pwani  Christopher Myava akizungumza na waandishi wa Habari hawapo pichani  Ofisini kwake leo Kibaha.



Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...