Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amefungua Tamasha la Utalii "Chato Utalii Festival 2023" linalofanyika wilayani Chato, mkoani Geita kwa lengo la kuhamasisha shughuli za utalii na kutangaza fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo mkoani humo.

Akizungumza wakati akifungua tamasha hilo Novemba 26, 2023 ambalo linaambatana na maonesho mbalimbali ya fursa zilizopo mkoani humo, alisema tamasha hilo limebeba dhana mbalimbali za uwekezaji hasa kwa upande wa kilimo, mifugo na uvuvi, utalii, utamaduni na michezo.

Alisema fursa za uwekezaji zilizopo katika Wilaya ya Chato ni nyingi huku akiwahimiza wananchi na wawekezaji mbalimbali kuzitumia  ili ziweze kuwaletea ufanisi na kukuza uchumi wa nchi na mtu mmoja mmoja.

Aidha, Waziri Ulega alitumia fursa hiyo kutaja maeneo mbalimbali ambayo yana fursa za uwekezaji mkoani humo huku akibainisha kuwa katika sekta ya uvuvi pekee Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa jumla ya shilingi Bilioni 1.7 kwa ajili ya kujenga mwalo na soko kubwa la kisasa la samaki wilayani chato ambalo litatoa fursa za kibiashara na uongezaji thamani wa mazao ya samaki na dagaa.

Halikadhalika, aliongeza kwa kusema kuwa Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa takriban shilingi Bilioni 1.8 kwa ajili ya kufanya  ujenzi wa kituo kikubwa cha  kuzalisha vifaranga vya samaki cha Rubambagwe kilichopo wilayani Chato ambacho kitawezesha wafugaji wa samaki kwa njia ya vizimba katika ukanda wa Ziwa Viktoria kuwa na uhakika wa kupata vifaranga bora vya samaki.

Kwa upande wa sekta ya mifugo, Waziri Ulega alisema Wizara imejenga mnada wa mifugo wa kisasa wa Buzirayombo ambao unatoa fursa kwa wafugaji kufanya biashara zao za mifugo kisasa huku akifafanua kuwa kufuatia uwepo wa idadi nzuri ya mifugo kunatoa fursa nyingine ya kujenga kiwanda cha kuchakata nyama.

Fursa nyingine alizozibainisha Waziri Ulega ni pamoja ujenzi wa hoteli kubwa za hadhi ya nyota tatu hadi tano kwa kuwa viwanja vinapatikana katika wilaya ya Chato, Kilimo cha umwagiliaji  kwa kuwa sehemu kubwa ya wilaya ya Chato imezungukwa na maji ya Ziwa Victoria na ujenzi wa viwanda vya Nguo kutokana na kuwepo kwa kinu cha kuchambulia pamba.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega (wa pili kulia) akiwa na Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhe. Martine Shigella (katikati) na viongozi mbalimbali mkoani humo muda mfupi baada ya kufungua  Tamasha la Utalii " Chato Utalii Festival 2023" linalofanyika wilayani Chato, mkoani Geita Novemba 26, 2023.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega  akimkabidhi mmoja wa washindi wa mbio za baiskeli  katika Tamasha la Utalii " Chato Utalii Festival 2023" linalofanyika wilayani Chato, mkoani Geita Novemba 26, 2023.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...