Mashindano ya Gofu ya 'NBC Waitara Trophy 2024' yamehitimishwa kwa mafanikio makubwa huku mdhamini mkuu wa mashindano hayo, benki ya NBC ikiahidi kuendelea kuyaboresha zaidi mashindano hayo ili yaendelea kuwa chachu ya kukuza na kuendeleza vipaji vya mchezo wa golf, kutangaza utalii sambamba na kumuenzi muasisi wa mashindano hayo Mkuu wa majeshi Mstaafu, Jenerali George Waitara.

Mashindano hayo yaliyohitimishwa na muasisi wake Jenerali Waitara kwenye viwanja vya Klabu ya Gofu vya Lugalo Jijini Dar es Salaam jana yalihusisha washiriki takribani 122 kutoka ndani na nje ya nchi, ikishuhudiwa wachezaji wa klabu ya gofu Lugalo waking’ara zaidi huku mchezaji Boniface Japhet kutoka klabu hiyo akiibuka mshindi wa jumla wa mashindano hayo.

Akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi mbalimbali wa mashindano hayo, Jenerali Waitara pamoja na kuwapongeza washiriki na wadhamini wa mashindano hayo, alitoa wito kwa jamii kushiriki kwa wingi kwenye mchezo huo unaojiongezea umaarufu hapa nchini huku akiwasii wapuuzie dhana iliyojengeka kwa muda mrefu kuwa mchezo wa gofu ni mahususi tu kwa watu wenye kipato kikubwa kwenye jamii.

“Niwasihi sana wazazi muendelee kuwaruhusu watoto na vijana wenu wajitokeze kwa wingi kushiriki mchezo huu kwa kuwa mbali na sababu za kiafya pia umekuwa ukiambatana na fursa mbalimbali za kiuchumi kwa washiriki huku pia ukitoa wasaa kwa washiriki kukutana na watu wa aina mbalimbali ndani na nje ya nchi hatua ambayo imekuwa ikiwasaidia kufungua fursa mbalimbali za kijamii na kibiashara,’’ alisema.

Zaidi Jenerali Waitara alitoa wito kwa wadhamini wa mashindano mbalimbali ya mchezo huo yakiwemo mashindano hayo kuangalia namna ya kupanua udhamini wao mbali na mashindano pekee pia waone namna ya kuboresha viwanja vya mchezo huo hususani kwenye mfumo wa umwagiliaji ili viweze kuwa katika hali nzuri hata kwenye msimu wa ukame.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Idara ya Wateja wadogo na Binafsi wa benki ya NBC, Bw Elibariki Masuke, Mkuu wa Idara ya Bima, Benki ya NBC Bw Benjamin Nkaka alisema ushiriki wa benki hiyo kwenye mashindano hayo kwa kiasi kikubwa unasukumwa na adhma ya benki hiyo katika kukuza na kuendeleza sekta ya michezo nchini ili kuibua vipaji, kuchochea ajira kupitia michezo pamoja na kuitumia vema sekta hiyo katika kutangaza utalii wa ndani.

“Kwetu mchezo wa gofu tunautazama kama moja ya michezo ya kimkakati inayoweza kulitangaza zaidi taifa hili huku pia ukitoa fursa kwa makundi tofauti ya wana jamii kuweza kujijengea fursa tofauti zikiwemo zile za kiuchumi bila kujali umri, jinsia au daraja lolote kiuchumi.Tumeamua kuunga mkono jitihada za muasisi wa mashindano haya Jenerali Waitara tukitambua hilo. Tunaahidi kuendeleza uhusiano wetu huu mzuri kupitia mashindano haya ili yaweze kutimiza malengo ya kuanzishwa kwake,’’ alisema Nkaka.

Akizungumzia mashindano hayo, Meneja wa Klabu ya Jeshi la Ulinzi la wananchi Wa Tanzania ya Lugalo-JWTZ Kanali David Mziray alisema licha ya kufanyika kwa mafanikio imeshuhudiwa washiriki mbalimbali wakiwemo watoto wakifanya vizuri zaidi kwenye mashindano hayo kwa kupata alama nzuri zaidi hatua ambayo inawakikishia ujio wa vipaji bora zaidi katika wakati mfupi ujao.

“Kupitia mashindano haya tumeshuhudia watoto wakifanya vema zaidi kwenye baadhi ya maeneo kiasi ambacho alama zao zinatoa changamoto kwa wakubwa hususani kwenye eneo kama upigaji wa mipira mirefu, hatua ambayo inatuonyesha mwanga mzuri huko tuendapo. Katika kuhakikisha hili linafanikiwa klabu yetu ya Lugalo tunatoa mafunzo ya mchezo wa gofu kwa watoto bure katika siku zote za Jumamosi,’’ alibainisha.

Kwa upande wao Rais wa Chama cha Gofu Tanzania (TGU), Gilman Kasiga na Rais wa chama cha gofu cha wanawake Tanzania (TLGU), Queen Siraki pamoja na kuonyesha kuvutiwa kwao na mafanikio makubwa ya mashindano hayo yanayoboreshwa kila mwaka walivutiwa zaidi na ongezeko kubwa la ushiriki wa wanawake na Watoto kwenye mashindano hayo hatua ambayo walisema inathibitisha muamko wa wana jamii katika kuupokea mchezo huo.

“Hata hivyo ushiriki wa ‘seniors’ sio mzuri sana hivyo tunaomba vilabu vione ipo haja ya kuanzisha mashindano maalumu kwa ajili ya seniors ili kuchochea ushiriki wao sambamba na kutoa fursa ya wao kukutana na kukumbushana mambo mbalimbali…hiyo ni miongoni mwa malengo ya mchezo huu,’’ alisema Kasiga.



Mkuu wa majeshi Mstaafu na Muasisi wa mashindano ya Gofu ya NBC Waitara Trophy, Jenerali George Waitara (wa pili kulia) akikabidhi zawadi ya kikombe na fedha taslimu kwa mshindi wa jumla wa mashindano ya NBC Waitara Trophy 2024 Boniface Japhet (wa pili kushoto) kutoka klabu ya gofu ya Lugalo. Mashindano hayo ya siku moja yalifanyika jana kwenye viwanja vya Klabu ya Gofu vya Lugalo Jijini Dar es Salaam kwa udhamini wa benki ya NBC yakihusisha washiriki takribani 122 kutoka ndani na nje ya nchi. Wanaoshuhudi ni pamoja na Mkuu wa Idara ya Bima, Benki ya NBC Bw Benjamin Nkaka (wa tatu kushoto), Rais wa chama cha gofu cha wanawake Tanzania (TLGU), Queen Siraki (kushoto) na Meneja wa Klabu ya Jeshi la Ulinzi la wananchi Wa Tanzania ya Lugalo-JWTZ Kanali David Mziray (Kulia).



Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ni alikuwa mmoja wa wakishiriki wa mashindano ya Gofu ya NBC Waitara Trophy.


Akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi zawadi kwa washindi mbalimbali wa mashindano hayo, Jenerali Waitara (pichani) pamoja na kuwapongeza washiriki na wadhamini wa mashindano hayo, alitoa wito kwa jamii kushiriki kwa wingi kwenye mchezo huo unaojiongezea umaarufu hapa nchini huku akiwasii wapuuzie dhana iliyojengeka kwa muda mrefu kuwa mchezo wa gofu ni mahususi tu kwa watu wenye kipato kikubwa kwenye jamii.





Akizungumza kwenye hafla hiyo Mkuu wa Idara ya Bima, Benki ya NBC Bw Benjamin Nkaka (pichani) alisema ushiriki wa benki hiyo kwenye mashindano hayo kwa kiasi kikubwa unasukumwa na adhma ya benki hiyo katika kukuza na kuendeleza sekta ya michezo nchini ili kuibua vipaji, kuchochea ajira kupitia michezo pamoja na kuitumia vema sekta hiyo katika kutangaza utalii wa ndani.






Mwalimu wa mchezo wa golf kutoka klabu ya Lugalo Abdallah Sanzagala (Pro Dullah) akiwaelekeza baadhi ya wafanyakazi wa benki ya NBC namna bora ya kucheza mchezo huo. Anaeshuhudia ni Mkuu wa Idara ya Bima, Benki ya NBC Bw Benjamin Nkaka (Kulia) ambae ni moja ya wachezaji vinara wa mchezo huo.



Karibu ushiriki NBC Waitara Trophy 2024!





Mkuu wa majeshi Mstaafu na Muasisi wa mashindano ya Gofu ya NBC Waitara Trophy, Jenerali George Waitara (katikati) akikabidhi zawadi ya fedha taslimu kwa washindi mbalimbali wa mashindano ya NBC Waitara Trophy 2024. Mashindano hayo ya siku moja yalifanyika jana kwenye viwanja vya Klabu ya Gofu vya Lugalo Jijini Dar es Salaam kwa udhamini wa benki ya NBC yakihusisha washiriki takribani 122 kutoka ndani na nje ya nchi.

Mashindano hayo yaliyohitimishwa na muasisi wake Jenerali Waitara kwenye viwanja vya Klabu ya Gofu vya Lugalo Jijini Dar es Salaam jana yalihusisha washiriki takribani 122 kutoka ndani na nje ya nchi, ikishuhudiwa wachezaji wa klabu ya gofu Lugalo waking’ara zaidi huku mchezaji Boniface Japhet kutoka klabu hiyo akiibuka mshindi wa jumla kwenye mashindano hayo.


Muonekano wa kikombe cha mshindi wa jumla wa mashindano ya Gofu ya NBC Waitara Trophy 2024. Boniface Japhet kutoka klabu ya gofu ya Lugalo aliibuka mshindi wa jumla wa mashindano hayo.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...