Na Derek MURUSURI, Dodoma


SHIRIKA la Utangazaji Tanzania litaendelea kutoa fursa sawa kutangaza kampeni za vyama vyote vitakavyoshiriki uchaguzi wa mwaka huu na mwaka 2025.

"Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020, TBC ilifuata ratiba ya kampeni ya vyama vya siasa, na kwingine TBC walifika na vyama vyenyewe havikufika," alisema Mhandisi Andrew Kisaka, Meneja wa Kitengo cha Mawasiliano cha TCRA.

Mhandishi Kisaka alikuwa akijibu hoja ya Mwanahabari na Mkuu wa Wilaya Mstaafu, Jenerali Ulimwengu.

Mwanahabari huyo, aliitaka TBC isichukue matangazo ya biashara kwa vile inafadhiliwa na Serikali na kuwataka watoe fursa sawa kwa vyama vyote vya siasa kwenye kipindi cha uchaguzi mkuu.

"Ni kweli TBC ni Shirika la Utangazaji la Umma na linaendelea kuchukua matangazo kwa sababu bado funding (ufadhili) yake haijakidhi viwango vya kuwa public broadcaster, lakini funding yake inafanyiwa kazi," alisema Mhandisi huyo.

Mhandisi Andrew Kisaka alisema hayo katika Kongamano la siku moja la wadau wa Habari na Uchaguzi, lililoandaliwa na Baraza la Habari Tanzania (MCT) katika Hoteli ya Dodoma jana (30 April, 2024).

Katika Uchaguzi wa mwaka 2020, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), waliwafukuza TBC katika mkutano wao wa kampeni.



Madhumuni


Akielezea madhumuni ya Kongamano hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa MCT, Bw Ernest Sungura, alisema kuwa waliwaleta pamoja wadau wa habari ili kujadiliana na kuweka mikakati ya pamoja katika kuongeza uwazi, haki na uwajibikaji tunapoelekea katika chaguzi za mwaka huu na 2025.


"Dira ya MCT ni kuchangia ukuaji wa demokrasia ya Tanzania kupitia uchaguzi wa viongozi kwa sanduku la kura na kujenga jamii ya haki," alisema Bw Sungura.

Manufaa ya Kongamano

Kongamano hilo lililofadhiliwa na Ubalozi wa Marekani nchini pamoja na Shirika la Kimataifa linalohusika na masuala ya Uchaguzi (IFES), lilikuwa na manufaa manne.

Kwanza ni kukuza maadili ya kidemokrasia kutokana na kujenga misingi ya
HAKI, UWAZI na UWAJIBIKAJI.

Pili, ni kuimarisha uhuru wa kutoa maoni kupitia
vyombo vya habari.

Manufaa mengine ni kuongeza elimu kwa wapiga kura itakayowasaidia kufanya maamuzi sahihi namakini katika sanduku la kupiga kura.

Mwisho, Bw Sungura alisema ni kuimarisha ushirikiano na kuaminiana miongoni mwa wadau muhimu wa uchaguzi.

"Hii ni pamoja na kuongeza imani kwa umma kutokana na
uandishi wa Habari usioficha kitu na usioegemea upande mmoja, unaotoa taarifa sahihi na za ukweli," alisisitiza.

Kongamano hilo la kwanza kufanyika nchini, lilihudhuriwa na washiriki mbalimbali kutoka vyombo vya habari pamoja na wadau wa Habari na uchaguzi.

Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu, Jaji Joseph Sinde Warioba, ndiye aliyekuwa Mgeni Rasmi.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...