Na PATRICIA KIMELEMETA

KUNA baadhi ya watoto wanazaliwa wakiwa na ulemavu wa aina mbalimbali huku baadhi yao ulemavu wao ukionekana kuanzia miezi sita na kuendelea ambapo mzazi au mlezi anatakiwa kumpeleka hospitali ili afanyiwe uchunguzi wa kina na kupatiwa matibabu.

Vitamini D ni muhimu kwa watoto kwa ajili ya kusimamia kiasi cha kalsiamu na fosforasi katika mwili na ni muhimu kwa ukuaji na matengenezo ya mifupa, meno na misuli. Kwa maneno mengine, vitamini D ni muhimu sana kwa afya ya mfupa na misuli kwa mtoto.

Vitamin D inaweza kupatikana kwa njia tatu: ikiwamo njia ya uzalishaji wa mwili kutokana na jua, kupitia chakula (hasa samaki au mafuta ya samaki) na kupitia virutubisho.

Mtoto akizaliwa na upungufu wa vitamin D mwilini inaweza kusababisha kuwa mifupa laini huku wengine wakipata ulemavu ambao ukiwahishwa hospitali unatibika.


Kutokana na uelewa duni wa baadhi ya wazazi, umechangia watoto wenye ukosefu wa vitamin D kudhaniwa kuwa ni walemavu na hawawezi kupona na wazazi au walezi kulazimiaha kutafita matibabu mbadala ( hata baadhi waganga wa kienyeji) wakiamini watawasaidia,jambo ambalo sio kweli.

Aisha Juma alijifungua mtoto akiwa na uvimbe shingoni, kadri mtoto alivyokua anakua, ndipo uvimbe ule uliendelea kuongezeka, awali hawakujua chanzo cha tatizo na kwamba walidhani ni ulemavu kama walivyo watoto wengine wenye ulemavu.

Licha ya kuangaika huku na huko jamii ilimuona kama mtoto mwenye ulemavu na kwamba hawezi kupona hata akifanyiwa matibabu.

Lakini cha ajabu ni kwamba, hata mumewe nae alimkimbia na kumuachia mtoto wa umri wa miaka miwili, jambo ambalo lilisababisha kuishi maisha magumu huku akiendelea kuangaika na mtoto wake.


" Mwanzo nilidhani nimejifungua mtoto mwenye ulemavu kutokana na kibiongo alichokua nacho na kama unavyojua jamii yetu uelewa mdogo, kila mmoja alisema lake, wakiwamo ndugu, jamaa na marafiki na hata baadhi wakinambia mwanao kalogwa.

" Nilienda kwa mganga kwa ajili ya kuangalia tatizo nini, lakini sijapata majibu, kadri anavyokua ndio ulemavu unazidi kuongezeka, mwisho mume wangu alinikimbia na huku akiniacha naangaika na mtoto peke yangu," amesema Aisha.

Akisimulia Aisha amesema kuwa, siku moja mtoto wake alikua anaumwa, akalazimika kumpeleka kwenye zahanati ya Chanika iliyopo Manispaa ya Ilala ambapo alikutana na muuguzi ambaye alimshauri ampeleke hospitali ya rufaa kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa kina.

" Nilimkubalia lakini sikua na uhakika kama mwanangu atapona, niliondoka kwenda hospitali kama aliyonielekeza na alipofanyiwa vipimo ilibainika mtoto alizaliwa akiwa na ukosefu wa vitamin D ambao ulisababisha kupata kibiongo ambacho mwanzo tulidhani ni uvimbe.

" Madaktari walimfanyia operesheni mwanangu na sasa hivi yupo kama watoto wengine waliozaliwa bila ya matatizo huku akiwa na afya njema, jambo ambalo mwanzoni sikutegwmwa kama mwanangu angepona,"amesema.

Aliwataka wazazi na walezi kuwapeleka watoto hospitali ili waweze kufanyiwa vipimo pale wanapoona kuna tatizo ili waweze kupatiwa matibabu mapema na sio kudharau na kudhani kuwa amelogwa, jambo ambalo linaweza kumsababishia mtoto kupata ulemavu unaoweza kutibika.

Ofisa Lishe Mtafiti kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe nchini (TFNC), Doris Katana amesema kuwa, siku 1000 ambazo huhesabiwa tangu siku mimba inapotungwa hadi mtoto anapotimiza miaka 2 ni siku muhimu kwa mama mjamzito na mtoto kula vyakula vyenye virutubisho ii kumjenga mtoto hasiweze kuzaliwa na changamoto mbalimbali za kiafya ikiwamo ukosefu wa vitamin D ambayo pia unaweza kupatikana kwenye samaki.

Amesema kuwa, mtoto anapotimiza umri wa miezi sita ananza kula vyakula mchanganyiko huku akiendelea kunyosha maziwa ya mama, hivyo basi anapaswa kutengenezwa vyakula vyenye virutubisho vyote ikiwamo samaki kwa wingi ili aweze kuimariaha afya yake.

" Mtoto anapokosa lishe bora kuanzia tumboni madhara yake ni makubwa ambapo anaweza kupata Utapiamlo, upungufu wa vitamin D mwilini ambayo unaweza kumsababishia kupata ulemavu na madhara meng," amesema Katana.

Amesema kuwa, imethibitika kuwa lishe bora katika kipindi hiki maalum cha Siku 1000, inaokoa maisha ya watoto zaidi ya milioni moja kila mwaka na uwezekano wa kupata magonjwa sugu yasiyoambukiza kama kisukari, saratani na magonjwa ya moyo ukubwani.

"Ni muhimu jamii kujali afya ya mama wakati wa ujauzito na wakati wa kunyonyesha kwa afya ya mtoto wake, lishe bora na mazingira safi na kuishi bila msongo wa mawazo ili kuboresha ukuaji wa mtoto kimwili na kiakili lakini pia hisia za mtoto zinachangiwa na lishe ya mama na maisha anayopitia wakati wa ujauzito," amesema.

Ameongeza kuwa, madhara ambayo anaweza kupata mama mjamzito au mtoto ndani ya sku 1000 ni pamoja na upungufu wa Vitamin D mwilini, upungufu wa wekundu wa damu, ukosefu wa madini joto na kutokuongezeka uzito.


Naye Daktari Bingwa wa watoto kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Honesta Kipatika amesema kuwa, watoto anatengeneza vitamin D kuanzia tumboni kwa mama yake, ikiwa mama mjamzito hana vitamin D ya kutosha mwilini inaweza kumletea madhara mtoto.

"Tafiti nyingi zinaonyesha kuwa, magonjwa mengi ya watoto yanatokana na upungufu wa vitamin D, sio tu mifupa kuwa dhaifu, lakini mtoto anaweza kuzaliwa na uzito pungufu, usonji, kupata maambukizi ya virusi na bakteria, saratani, magonjwa ya moyo na hata mama mjamzito kupata kifafa cha mimba ," amesema. Dk. Kipatika.

Amesema kuwa, mtoto anapozaliwa kuna kiasi cha vitamin D kinahitajika ambacho linatokana kwa mama yake na nyiingine ataipata Kwa njia ya kunyonyeshwa Ili kuimariaha ukuaji wa afya yake ya mwili na ubongo.

Amesema kuwa, madhara ya mtoto kukosa vitamin D ni pamoja na kudumaa, mifupa yake kuvunjika mara kwa mara, kupata maambukizi ya virusi na bakteria, kifua na matatizo mengine ambayo yatarudisha nyuma ukuaji wake.

Amesema kuwa, baadhi ya watoto wanaanza kuonyesha dalili wakiwa na miezi sita na kuendelea, hii inatokana na Haina ya ukuaji wake, utaona mwili dhaifu, wana matege, ngozi dhaifu,wanaumwa mara kwa mara na hata baadhi yao kupata upungufu wa damu.

Amesema kuwa, kutokana na hali hiyo, kuanzia mtoto anapotimiza umri wa mwaka 1-3 anahitaji kupata vitamin D ya kutoaha ili aweze kukua katika hali ya utimilifu, samaki.

" Mzazi ukiona umejifungua mtoto hayupo sawa mpeleke hospitali kufanyiwa vipimo ili aweze kupata matibabu ya haraka, kwa sababu baadhi ya magonjwa kwa mtoto yanatibika, ukijifungua hakikisha unamkagua mtoto wako mara kwa mara ili uweze kubaini tatizo alilonalo na kumuwaisha hospitali kwa ajili ya matibabu kwa sababu mifupa ya mtoto mchanga ni laini," amesema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Taasisi inayojishughulisha na watoto wenye ulemavu ya Kaya Foundation,Anapili Ngome amesema kuwa, baadhi ya wazazi (kina baba) wanapoona mkewe amejifungua mtoto mwenye changamoto ya viungo, wana tabia ya kuwakimbia na kusababisha mtoto kulelewa na mzazi mmoja kwenye mazingira magumu.

" Kina baba hampaswi kukwepa majukumu ya malezi kwa watoto wenu, kama mlivyoahirikiana kumtafuta, mnapaswa kushirikiana kumlea kwa sababu mtoto anahitaji upendo kutoka kwa wazazi wote wawili na jamii husika," amesema Ngome.

Ameongeza mtoto anapozaliwa na ulemavu ana haki sawa kama ilivyo mtoto asiye na ulemavu, anahitaji usaidizi wa karibu kutoka kwa jamii, kitendo cha kumnyanyapaa kinachangia kumrudisha nyumba kwenye malezi yake, hivyo basi kila mmoja ana wajibu wa kuhakikisha anashiriki kwenye malezi ya mtoto ipasavyo.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...