-Ahimiza mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita kutangazwa kwa wananchi

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amevitaka vyombo vya habari vinavyomilikiwa na chama hicho kuzingatia weledi, hasa kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Balozi Nchimbi amesema vyombo hivyo vina wajibu mkubwa wa kutumia weledi huo kutangaza mafanikio makubwa ya Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza Alhamisi, tarehe 5 Juni 2025, wakati wa kikao na baadhi ya wakuu wa idara wa vyombo vya habari vya CCM, wakiongozwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu Mtendaji wa Uhuru Media Group (UMG), Dennis Msacky, Balozi Nchimbi alisisitiza kuwa weledi wa vyombo hivyo uendelee kuwa mfano wa kuigwa katika tasnia ya habari nchini.

Mazungumzo hayo yalifanyika katika Ofisi Ndogo za Makao Makuu ya CCM, Lumumba, jijini Dar es Salaam, ambapo pia aliwapongeza kwa namna wanavyoendelea kuwahabarisha wananchi kuhusu masuala yanayohusu Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

Balozi Nchimbi alisema vyombo hivyo vya habari, ambavyo ni sauti ya chama, vina jukumu la kuutangazia umma utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati chini ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020–2025, sambamba na kuanza kuchambua Ilani mpya ya chama hicho kwa mwaka 2025–2030.

Kwa upande wao, wawakilishi wa vyombo hivyo walieleza namna walivyojipanga kufikisha taarifa kwa jamii, zikiwemo elimu ya uraia kuelekea uchaguzi, namna ya kushiriki, na mchakato wa kuwapata wagombea bora ndani ya CCM, kwa lengo la kuhakikisha chama hicho kinapata ushindi wa kishindo. 









Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...