Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa kwa wadau wote wa mazingira kuendeleza mambo yote yaliyofanyika katika maadhimisho ya mazingira ikiwa ni pamoja na upandaji miti na uanzishwaji wa bustani za kijani.
Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani iliyofanyika Kitaifa katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete Mkoani Dodoma. Amewahimiza wadau hao kuhamasisha matumizi ya teknolojia za urejelezaji wa taka ozo na za plastiki, kupunguza ukataji miti holela kwa ajili ya kuni na mkaa na kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Aidha, Makamu wa Rais amesema Serikali imeweka nia ya kupunguza athari za uharibifu wa mazingira kwa kupunguza matumizi ya nishati ya kuni na mkaa kwa shughuli za kupikia. Amesema katika kutekeleza nia hiyo, Serikali ilitoa katazo la matumizi ya kuni na mkaa kwa taasisi zinazoandaa chakula na kulisha watu zaidi ya watu mia moja kwa siku na kuzitaka zihamie katika matumizi ya nishati safi ya kupikia ambapo kufikia Machi 2025 jumla ya taasisi 762 zimeanza kutumia nishati safi ya kupikia kati ya hizo taasisi za umma ni 495 na taasisi binafsi ni 267.
Halikadhalika Makamu wa Rais amesema jukumu la kuhamasisha na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa hifadhi ya mazingira linahitaji ushirikiano wa wadau wote katika ngazi zote. ametoa wito kwa vyombo vya habari, taasisi zote za Serikali, binafsi na asasi za kiraia kushirikiana katika kutoa elimu kwa jamii ili kupunguza uharibifu wa mazingira hapa nchini kwa kiasi kikubwa.
Makamu wa Rais amesema taarifa mbalimbali za hali ya mazingira nchini zimedhihirisha kuwepo kwa uharibifu wa ardhi katika maeneo mbalimbali nchini, ambapo inakadiriwa kuwa takriban asilimia 61 ya ardhi nchini iko katika hatari ya kuharibika. Amesema uharibifu huo unachangiwa kwa kiasi kikubwa na shughuli za kibinadamu zisizo endelevu, idadi kubwa ya mifugo isiyolingana na uwezo wa malisho, ukataji wa misitu kwa ajili ya kuni na mkaa, uanzishaji wa mashamba mapya unaotokana na kilimo cha kuhamahama, uchimbaji holela wa madini pamoja na upanuzi wa makazi usiozingatia mipango miji.
Makamu wa Rais amesema katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira, Serikali imechukua hatua mbalimbali za kisera na kimkakati ikiwa ni pamoja na kupitishwa kwa Sera ya Taifa ya Mazingira ya mwaka 2021, Mpango Kabambe wa Taifa wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022-2032), kuongeza kasi ya upimaji wa ardhi na umilikishaji wa ardhi kimila.
Amesema hatua nyingine ni pamoja na uhamasishaji wa matumizi endelevu ya ardhi hususan kilimo mseto, kilimo cha matuta, kilimo hifadhi na mbinu endelevu za kiasili za hifadhi ya malisho. na utekelezaji wa hatua hizi ikiwa ni pamoja na kuendelea kuhamasisha utunzaji wa mazingira kwa ujumla.
Vilevile, Makamu wa Rais amewahimiza wananchi kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwan kwa kugombea nafasi mbalimbali za uongozi, kushiriki kampeni ili kusikiliza sera za wagombea na kujitokeza kupiga kura siku ya uchaguzi. Aidha amewasihi wananchi hususani vijana kudumisha hali ya utulivu na usalama hususan katika hatua ya uteuzi wa wagombea, kampeni za uchaguzi, upigaji kura na hata baada ya matokeo kutangazwa.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Khamis Hamza Khamis amesema kauli mbiu ya mwaka 2025 inahamasisha jamii kupunguza matumizi ya bidhaa za plastiki kwa kuwa na uzalishaji na ulaji endelevu kwa lengo la kuhifadhi mito, maziwa na bahari ili kuhifadhi mifumo ya ikolojia.
Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani Kitaifa yamebeba kauli mbiu isemayo “Mazingira Yetu na Tanzania Ijayo, Tuwajibike Sasa: Dhibiti Matumizi ya Plastiki”.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...