Na Mwandishi Wetu – Dodoma 04 Juni 2025 

Mamia ya wananchi wamejitokeza katika banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kupata huduma mbalimbali za kielimu na kiafya wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Mazingira Duniani yanayoendelea jijini Dodoma.

Miongoni mwa vivutio vikubwa katika banda hilo lililoko viwanja vya Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete (JKCC), ni huduma ya tiba ya kuimarisha kinga ya mwili kwa kutumia nyuki (api-therapy), iliyokuwa ikitolewa na Mhifadhi Brenda Mwakipesile kutoka TFS.

Mwakipesile alisema tiba hiyo ya asili inasaidia kuchochea kinga ya mwili na kutoa ahueni kwa baadhi ya maumivu ya muda mrefu, hasa ya viungo.

“Tiba hii inatumia sumu ya nyuki kwa njia salama na inayodhibitiwa, na imekuwa na matokeo chanya kwa baadhi ya wagonjwa waliowahi kuipokea. Leo tumeona muitikio mkubwa wa wananchi walio na shauku ya kujifunza na kupata huduma hii,” alisema.

Mbali na huduma hiyo, TFS ilitoa elimu kwa wananchi kuhusu uhifadhi wa misitu, matumizi ya nishati safi ya kupikia, uzalishaji wa mkaa mbadala, upandaji wa miti na utunzaji wa vyanzo vya maji.

Maonesho haya yamebeba kaulimbiu: “Mazingira Yetu na Tanzania Ijayo, Tuwajibike Sasa – Dhibiti Matumizi ya Plastiki”, yakihusisha taasisi mbalimbali za Serikali, mashirika ya kimataifa, sekta binafsi na wananchi.
Wananchi waliotembelea banda la TFS walionesha kufurahishwa na huduma na elimu waliyoipata, wakieleza kuwa ni tofauti na ilivyozoeleka katika maonyesho mengine.

“Nimejifunza mengi kuhusu misitu, lakini pia sikuwahi kufikiria nyuki wanaweza kutumika kama tiba. Ni jambo jipya na la kuvutia sana,” alisema Rehema John, mkazi wa Dodoma.

Maadhimisho ya Wiki ya Mazingira yanatarajiwa kufikia kilele chake Juni 5, yakilenga kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira kwa mustakabali wa Taifa.




 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...