“JK na Dar City Afrika Kusini”
Rais Mstaafu Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jopo la Wazee la Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC Panel of Elders - POE), na Mwakilishi wa Ngazi ya Juu wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika katika juhudi za kutatua mgogoro wa Sudan Kusini, amekutana leo na timu ya mpira wa kikapu ya Dar City inayoshiriki Michuano ya Ligi ya Mpira wa Kikapu Afrika (Basketball Africa League (BAL) 2026, inayoendelea jijini Pretoria, Afrika Kusini.
Katika mazungumzo na timu hiyo iliyoambatana na Rais wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF), Hasheem Thabit pamoja na Viongozi wengine kutoka Serikalini, Rais Mstaafu Dkt. Kikwete ameipongeza Timu ya Dar City kwa kufikia hatua hiyo muhimu ya mashindano, akieleza kuwa mafanikio hayo ni ishara ya kukua kwa kiwango cha mpira wa kikapu nchini Tanzania.
Aidha, amewatia moyo na kuwapa ari wachezaji ya kupambana katika mchezo wao mmoja uliosalia kabla ya kufika fainali, akisisitiza umuhimu wa nidhamu, kujituma na kujiamini wanapoingia uwanjani. "Kwa hatua mliyofikia, nina imani kabisa mnaweza kutinga fainali na hatimaye kubeba kombe hili, labda itokee miujiza", alisema Dkt. Kikwete akizungumza na wachezaji hao.
Rais Mstaafu Dkt. Kikwete, ambaye amewahi kuwa mlezi wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF) huku akiwa mstari wa mbele katika kuendeleza mchezo huo wakati wa uongozi wake, ametumia fursa hiyo pia kutoa pongezi kwa dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa unaofanyika katika sekta ya michezo nchini. Aidha, ameipongeza Wizara yenye dhamana ya kusimamia Michezo pamoja na Shirikisho la TBF kwa kusimamia vizuri maendeleo ya mpira wa kikapu, huku akibainisha kuwa mafanikio ya timu ya Dar City ni mojawapo ya matunda ya Serikali kuwekeza katika michezo.
Mheshimiwa Dkt. Kikwete yupo nchini Afrika Kusini kwa ziara ya kikazi ambapo amekutana na Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, kama sehemu ya kutekeleza majukumu yake ya kikanda akiwa kama Mwenyekiti wa Jopo la Wazee la SADC, pamoja na jukumu lake jipya chini ya Umoja wa Afrika la kusaidia kutafuta suluhu ya mgogoro wa Sudan Kusini.



.jpeg)


Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...