Na Ruth Kyelula, Manyara

Mkoa wa Manyara unatarajia kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani kimkoa tarehe 8 Machi 2026 katika Wilaya ya Simanjiro, huku Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Queen Sendiga, akitoa wito kwa jamii kuhakikisha haki za wanawake na wasichana zinalindwa na kuheshimiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Machi 3, 2026 ofisini kwake mjini Babati, Sendiga alisema maadhimisho hayo ni fursa muhimu ya kuhamasisha jamii kushiriki katika juhudi za kukuza usawa wa kijinsia, kuwawezesha wanawake kiuchumi na kuimarisha ustawi wao katika jamii.

Alisema Mkoa wa Manyara umekuwa ukikabiliwa na changamoto ya matukio ya ukatili wa kijinsia, lakini juhudi mbalimbali zimeendelea kufanyika ili kukabiliana na tatizo hilo. Alisisitiza kuwa wazazi na jamii kwa ujumla wanapaswa kuhakikisha watoto, hususan wasichana, wanapata haki zao na kulindwa dhidi ya vitendo vya ukatili.

Sendiga alieleza kuwa chimbuko la Siku ya Wanawake Duniani linatokana na harakati za wanawake wafanyakazi waliopigania haki zao kazini, jambo linaloifanya siku hiyo kuwa jukwaa la kuhimiza uwajibikaji kwa wanawake pamoja na kuwakumbusha waajiri, taasisi na serikali kuhakikisha mazingira ya kazi yanazingatia usawa wa mishahara, maslahi na fursa.

Aliongeza kuwa Tanzania imekuwa ikiadhimisha siku hiyo tangu mwaka 1997 kwa lengo la kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa, huku kaulimbiu ya mwaka huu ikiwa ni “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050.”

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...