Serikali ya Tanzania imesaini mkataba na Kampuni ya Lindi Jumbo Limited kwa ajili ya kuwezesha ushiriki rasmi wa Serikali katika Mradi wa uchimbaji wa madini ya kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, hatua inayotajwa kuwa mafanikio makubwa kwa sekta ya madini na mkakati wake kupitia ajenda ya madini nchini.
Hafla ya utiaji saini iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi, imeiwezesha Serikali kupata asilimia 16 ya hisa huru zisizohafifishwa thamani katika mradi huo, huku Lindi Jumbo Limited ikibaki na umiliki wa asilimia 84.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, alisema makubaliano hayo ni hatua ya kihistoria katika kuhakikisha Watanzania wananufaika moja kwa moja na rasilimali za taifa kupitia ushiriki wa Serikali katika uwekezaji wa madini.
Kwa mujibu wa makubaliano hayo, Serikali itashiriki katika mradi bila kubeba gharama za awali za uwekezaji, huku ikipata gawio, kushiriki katika maamuzi ya kimkakati pamoja na kuongeza usimamizi wa mapato yatokanayo na madini.
Mheshimiwa Mavunde alisema makubaliano hayo yanaonesha mabadiliko ya namna Tanzania inavyosimamia rasilimali zake za madini, akisisitiza kuwa nchi inapaswa kuondokana na utegemezi wa kuuza malighafi pekee.
“Serikali chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuimarisha taswira ya Tanzania kama eneo tulivu na rafiki kwa wawekezaji,” alisema. “Kupitia sheria zilizo wazi, taasisi zinazoendelea kuimarika na dira ya muda mrefu ya uchumi, wawekezaji sasa wanaiona Tanzania siyo tu kama chanzo cha madini, bali mshirika wa kuaminika katika uwekezaji wenye usawa na endelevu.”
Waziri huyo alieleza kuwa Kinywe imeendelea kuwa madini muhimu duniani kutokana na matumizi yake katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, teknolojia za nishati safi na mabadiliko ya mfumo wa matumizi ya nishati duniani.
Aliitaja Kinywe kama “dhahabu nyeusi” ya uchumi wa kisasa, akisema uchumi wa dunia utaendelea kutegemea madini mkakati yanayochochea maendeleo ya teknolojia na mifumo ya nishati ya kijani.
Kwa mujibu wa Mheshimiwa Mavunde, Mradi wa Lindi Jumbo ni miongoni mwa miradi yenye kiwango cha juu zaidi cha ubora wa kinywe duniani, ukiwa na wastani wa asilimia 17.9 ya Total Graphitic Carbon (TGC), hali inayoufanya kuwa moja ya migodi bora zaidi ya kinywe barani Afrika. Mradi huo unatarajiwa kuzalisha takribani tani 40,000 za kinywe kwa mwaka katika kipindi cha miaka 24 ya uhai wa mgodi.
Waziri huyo pia alisisitiza dhamira ya Serikali katika kuendeleza uchumi wa viwanda na kuongeza thamani ya madini, akisema Tanzania inalenga kuhamasisha uwekezaji katika uchakataji wa madini, utengenezaji wa betri na viwanda vinavyotegemea kinywe pamoja na madini mengine ya kimkakati.
Akihitimisha hotuba yake, Mheshimiwa Mavunde alisema Tanzania imejipanga kujenga sekta ya madini ya kisasa, thabiti na yenye ushindani wa kimataifa inayozingatia uwazi, uhakika na ushirikiano wa muda mrefu.
Alisema makubaliano hayo yanaashiria enzi mpya ya ushirikiano kati ya Serikali, wawekezaji na wananchi, yakionyesha kuwa uwekezaji, uzalendo na ukuaji wa uchumi vinaweza kwenda sambamba.
“Utajiri wa madini wa Tanzania lazima ugeuzwe kuwa ajira, viwanda, maarifa na matumaini kwa vizazi vijavyo,” alisema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, alisema utiaji saini wa makubaliano hayo ni ishara ya mafanikio ya safari ndefu ya maendeleo ya mradi huo pamoja na mwanzo wa hatua mpya ya ushirikiano na ukuaji wa sekta ya kinywe nchini Tanzania.
Bwana Cunningham alisema Mradi wa Lindi Jumbo ulianza zaidi ya miaka kumi iliyopita, huku shughuli za utafiti wa madini zikianza mwaka 2015 kwa lengo la kufungua fursa ya utajiri wa grafiti nchini Tanzania.
Alisema tangu wakati huo mradi huo umepitia hatua mbalimbali zikiwemo utafiti, tafiti za kitaalamu, upatikanaji wa fedha, ujenzi na uzalishaji hadi kufikia kuwa moja ya migodi bora ya kinywe duniani.
“Lindi Jumbo unakadiriwa kuwa na maisha ya mgodi ya miaka 24, huku ukiwa na uwezekano mkubwa wa kuongeza shughuli za uzalishaji hadi zaidi ya miaka 50 kutokana na utafiti unaoendelea,” alisema Bwana Cunningham. “Thamani ya mradi huu haipo tu katika muda wake mrefu wa uzalishaji, bali pia katika ubora mkubwa wa madini yake unaouweka katika nafasi nzuri katika soko la kimataifa la madini mkakati.”
Alisema kinywe imeendelea kuwa madini muhimu katika uchumi wa kisasa kutokana na matumizi yake katika shughuli za viwanda, teknolojia za kisasa na mifumo mipya ya nishati.
Kuhusu uzalishaji, mkurugenzi huyo alisema, mwaka 2025 mgodi huo ulisindika karibu tani kavu 170,000 za madini ghafi na kuzalisha tani 16,421 za kinywe yenye kiwango cha ubora kati ya asilimia 94 na 96 TGC.
Aliongeza kuwa mradi huo ulichimba zaidi ya tani 500,000 za mchanga na miamba katika kipindi hicho, huku oda za mauzo zilizothibitishwa zikizidi tani 27,800.
Bwana Cunningham pia alieleza mchango wa mradi huo kwa uchumi wa Tanzania, akisema kampuni ilitumia shilingi bilioni 57.5 kwa wazabuni wa ndani kati ya mwaka 2024 na 2025, ambapo asilimia 91 ya manunuzi yote yalielekezwa kwa kampuni za Kitanzania.
Aidha, kampuni hiyo ilichangia zaidi ya shilingi bilioni 11.3 kupitia mrabaha, kodi na malipo mbalimbali ya kisheria kwa Serikali.
Kwa mujibu wa Bwana Cunningham, mradi huo pamoja na wakandarasi wake unaajiri watu 280, ambapo zaidi ya asilimia 95 ni Watanzania, huku zaidi ya nusu ya wafanyakazi wakitoka vijiji vinavyozunguka Wilaya ya Ruangwa.
Pia alieleza juhudi za kampuni katika uwekezaji kwa jamii, akibainisha kuwa zaidi ya shilingi milioni 162 zimetengwa kwa ajili ya programu za uwajibikaji kwa jamii katika sekta za afya, elimu na maendeleo ya jamii.
Miongoni mwa miradi hiyo ni ujenzi wa zahanati katika Kijiji cha Namilema kwa lengo la kuboresha huduma muhimu za afya kwa wananchi wa maeneo yanayozunguka mradi huo.
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (wa pili kushoto), akishikana mikono na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, baada ya hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Wanaoangalia kutoka kulia ni Mwakilishi kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina, Emmanuel Luvanda; Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell; na Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa.
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (wa pili kushoto), akiwa na, kutoka kushoto, Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham; Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa; pamoja na Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell, wakionesha hati za mikataba, baada ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, akisaini nyaraka za makubaliano pamoja na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham (wa tatu kulia), na Mwakilishi wa Gemcorp, William Binedell (wa pili kulia), wakati wa hafla rasmi ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Kulia ni Mwanasheria na Katibu wa Kampuni ya Lindi Jumbo, Ephraim Mrawa.
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, akihutubia wakati wa hafla rasmi ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.
Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, akitoa shukrani baada ya hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa Kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde, alikuwa mgeni rasmi.
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (kushoto), akipokelewa na Mtendaji Mkuu wa Lindi Jumbo, Paul Lombar, kabla ya kuongoza hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa kampuni hiyo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.
Waziri wa Madini, Mheshimiwa Anthony Mavunde (kushoto), akipokelewa na Mkurugenzi wa Lindi Jumbo, Andrew Cunningham, alipoenda kuwa mgeni rasmi katika hafla ya utiaji saini wa makubaliano kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Lindi Jumbo Limited kuhusu ushiriki wa Serikali katika Mradi wa kinywe wa Lindi Jumbo kupitia kampuni ya ubia ya Ndovu Graphite Limited, iliyofanyika jana katika Kijiji cha Matambarale, Wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi. Wa pili kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Mohamed Moyo.

Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...