Na Mwandishi Wetu.
TANZANIA imefungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika sayansi, teknolojia na ubunifu baada ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kuingia katika ushirikiano na Kongani ya Ubunifu ya Incheon (Incheon Innovation Cluster—IIC) ya Korea Kusini.

Ushirikiano huo unalenga kuanzisha Tawi la IIC nchini Tanzania, hatua inayotarajiwa kuwaunganisha watafiti na wabunifu wa Tanzania na fursa za utaalamu, teknolojia, utafiti na biashara kutoka Korea Kusini.

Hafla ya utiaji saini wa Mkataba wa Makubaliano kati ya COSTECH na IIC imefanyika leo Septemba 3, 2026, katika Songdo Convensia, Incheon, Korea Kusini, ikiwa sehemu ya Mkutano wa Kimataifa wa Teknolojia za Mazingira wa Incheon 2026.

Akizungumza katika hafla hiyo, Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Noel Kaganda, alisema ushirikiano huo unapaswa kwenda zaidi ya Tanzania kupokea teknolojia kutoka nje.

“Tunapaswa kuachana na utamaduni wa kununua teknolojia zilizotengenezwa tayari na badala yake kuelekea katika kuzalisha teknolojia kwa pamoja, kuzijaribu kwa kuzingatia mazingira yetu na kuhakikisha zinaendana na mahitaji yetu,” alisema.

Kaganda alisema ubunifu unapaswa kuwa wa pande zote mbili, huku akisisitiza umuhimu wa Tanzania kushiriki katika mchakato wa kutengeneza na kuendeleza teknolojia.

“Ubunifu lazima uwe shirikishi. Hatupaswi kuwa na nchi moja inayozalisha na nyingine inayobaki kuwa mtumiaji pekee katika ikolojia ya ubunifu,” alisema.

Kupitia ushirikiano huo, watafiti na wabunifu wa Tanzania watapata nafasi ya kushirikiana na taasisi za utafiti, wataalamu na kampuni za Korea Kusini katika kuendeleza teknolojia na kuzifikisha katika matumizi ya kibiashara.

Mkataba huo unaainisha maeneo ya utafiti wa pamoja, maendeleo na uhamishaji wa teknolojia, ubunifu, ubia wa kibiashara pamoja na mikutano na programu za pamoja.

Fursa hiyo inatajwa kuwa muhimu kwa wabunifu ambao wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya kupeleka bunifu zao kutoka hatua ya wazo au mfano wa bidhaa hadi katika uzalishaji na soko.

Kwa upande mwingine, Korea Kusini itapata fursa ya kushirikiana na Tanzania katika kuelewa changamoto za ndani, ubunifu unaozalishwa nchini na fursa zilizopo katika soko la Tanzania na Afrika.

Akizungumzia umuhimu wa hatua hiyo, Kaganda alisema ushirikiano huo unaweza pia kuwa sehemu ya diplomasia ya sayansi, teknolojia na ubunifu kati ya Tanzania na Korea Kusini.

“Leo tunashuhudia utiaji saini wa Mkataba wa Makubaliano kati ya COSTECH na IIC. Huu ni ushahidi wa dhamira thabiti ya Serikali zetu katika kujenga diplomasia ya sayansi, teknolojia na ubunifu. Niwatake COSTECH na IIC kuendeleza diplomasia hii ya sayansi, teknolojia na ubunifu ili ushirikiano huu uweze kuleta matokeo yaliyokusudiwa kwa kiwango kikubwa,” alisema.

Ushirikiano huo pia unakuja wakati Serikali ya Tanzania ikisisitiza umuhimu wa kujifunza kutokana na uzoefu wa Korea Kusini katika kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu katika kujenga uchumi.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alitoa msukumo huo Julai 2, 2026, wakati wa uzinduzi wa shughuli za miaka 40 ya COSTECH, akitaka Tanzania kujifunza namna Korea Kusini ilivyotumia teknolojia na ubunifu katika mabadiliko yake ya kiuchumi.

Kwa wabunifu wa Tanzania, hatua hiyo sasa inaweka mezani swali la muhimu: ni bunifu zipi za Tanzania zitakazovuka mipaka na kupata nafasi katika mfumo wa teknolojia wa Korea Kusini?

Jibu lake litategemea uwezo wa COSTECH na IIC kubadili makubaliano hayo kuwa miradi halisi, utafiti wa pamoja, mafunzo, uhamishaji wa teknolojia, ubia wa biashara na fursa za soko kwa wabunifu wa Tanzania.

Hapo ndipo thamani halisi ya Tawi la IIC nchini Tanzania itakapopimwa.




Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...