Na Janeth Raphael - MichuziTv

Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) imewataka wataalamu wote waliosajiliwa ambao hawajalipa ada zao za mwaka kukamilisha malipo ya madeni yote ndani ya siku 30, ikionya kuwa watakaoshindwa kutekeleza agizo hilo wanaweza kuchukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria, ikiwemo kufutiwa usajili na majina yao kuchapishwa rasmi.

Mkurugenzi Mtendaji wa PSPTB, Godfred Mbanyi, ametoa kauli hiyo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa wajibu wa wataalamu waliosajiliwa na Bodi. Amesema hatua hizo zinalenga kuhakikisha wataalamu wanatimiza wajibu wao kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazosimamia taaluma ya ununuzi na ugavi nchini.

PSPTB ni taasisi ya Serikali iliyo chini ya Wizara ya Fedha, iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Bodi ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi, Sura ya 179 ya Sheria za Tanzania. Bodi ina jukumu la kusimamia na kudhibiti viwango, mwenendo na maadili ya taaluma hiyo, huku ikiwa na mamlaka ya kusajili watu wanaokidhi vigezo na kuwapa uhalali wa kufanya kazi za kitaaluma katika eneo hilo.

Bodi imekumbusha kuwa ulipaji wa ada ya mwaka ni wajibu wa kisheria kwa kila mtaalamu aliyesajiliwa, kwa mujibu wa kanuni zake, ikiwemo Tangazo la Serikali Na. 364 la mwaka 2009. Mtaalamu anayeshindwa kulipa ada hiyo kwa kipindi cha miezi 24 mfululizo anaweza kupoteza hadhi ya usajili na jina lake kuondolewa kwenye daftari rasmi la PSPTB.

Aidha, PSPTB imeonya kuwa mtu anayeendelea kufanya kazi, kujitambulisha au kujihusisha na taaluma ya ununuzi na ugavi bila kuwa amesajiliwa na Bodi anafanya kosa la jinai na anaweza kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria. Kwa mujibu wa Kifungu cha 46(2) na (3) cha Sheria ya PSPTB, Bodi ina mamlaka ya kuchukua hatua za kisheria na kinidhamu dhidi ya wanaokiuka masharti hayo.

Kwa hatua hiyo, PSPTB imewataka wataalamu wote wenye madeni ya ada ya mwaka kuhakikisha wamelipa madeni yao yote ndani ya siku 30 kuanzia tarehe ya tangazo hilo. Bodi imesisitiza kuwa watakaokaidi watachukuliwa hatua, ikiwemo kufutiwa usajili, kuchapishwa kwa majina yao na, pale inapobidi, kufunguliwa mashitaka kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha Bodi.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...