Waziri wa Viwanda na Biashara Mh. Abdallah Kigoda akifungua mkutano wa Kibiashara baina ya maafisa wa Serikali kutoka Taasisi mbalimbali nchini Tanzania na wafanyabiashara na wawekezaji wa Korea uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa hotel ya Lotte iliyoko jijini Seoul Korea Kusini.

Na: Geofrey Tengeneza- Seoul Korea Kusini.

Waziri wa Viwanda na Biashara Mh. Dakta Abdallah Kigoda ametoa rai kwa wafanyabiashara na wawekezaji nchini Korea kuja kuwekeza katika sekta mbalimbali za uchumi nchini Tanzania ikiwa ni pamoja na sekta ya utalii ambayo amesema ina fursa nyingi za uwekezaji katika Nyanja mbalimbali kama vile malazi, usafiri na usafirishaji watalii, utalii wa majini (cruise boat) na kadhalika.

Akizungumzia zaidi kuhusu utalii, Dk. Kigoda amewaambia wawekezaji hao kuwa Tanzania ni eneo bora la utalii kwani ni nchi yenye vivutio vizuri na vya aina yake barani Afrika, hivyo akawahimiza kuja kuitembelea na kujionea wenyewe kwa macho yao utajiri, uzuri na upekee wa vivutio hivyo vya utalii ukilinganisha na vile vinavyopatikana katika nchi nyingine Afrika na duniani kwa ujumla. 

Waziri Kigoda alitumia fursa hiyo kumpongeza mwanamuziki maarufu wa hapa Korea na mwenye washabiki wengi sana nchini hapa aliyejulikana kwa jina moja la Choy kwa kazi nzuri ya kuutangaza mlima Kilimanjaro nchini Korea kupitia sanaa ya muziki “Tanzania ina utajiri wa vivutio vingi vya utalii, kwa mfano mlima Kilimanjaro uko Tanzania, narudia kwa msisitizo kuwa uko Tanzania na si nchi nyingine yeyote, na nina mshukuru sana mwanamuziki Choy kwa kuutangaza mlima huo hapa Korea, alisema waziri Kigoda huku akishangiliwa kwa makofi.

Waziri Kigoda ameyasema hayo hivi karibuni jijini Seoul nchini Korea katika hotuba yake aliyoitoa wakati wa mkutano wa Kibiashara baina ya wafanyabiashara na wawekezaji wa kikorea takribani 100 kutoka katika sekta kadhaa chini Korea na ujumbe wa maafisa wa Serikali ya Tanzania kutoka sekta mbalimbali uliofanyika katika hotel ya Lotte na kuhuduriwa pia na jumuia ya watanzania wanaoishi nchini Korea. 

Alivitaja baadhi ya vivutio ambavyo Tanzania inajivunia kuwa ni pamoja na mlima Kilimanjaro ambao ni mrefu kuliko yote barani Afrika, Bonde la Ngorongoro ambalo ni maajabu ya nane ya dunia, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ambayo ni miongoni mwa maajabu mapya saba ya dunia na Visiwa vya Zanzibar ambavyo ni maarufu kwa utalii wa fukwe na maeneo ya Kihistoria. 

Pembezoni mwa mkutano huo kulikuwa pia na maonesho madogo ya utalii wa Tanzania ambapo wawekezaji hao walipatiwa pia vielelezo kadhaa vya utalii sambamba na maelezo yaliyokuwa yakitolewa na maafisa kutoka Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) na Mamlaka ya hifadhi ya bonde la ngorongoro (NCAA).

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 3 mpaka sasa

  1. Juhudi kama hizi japo ni muhimu sana zikafanyika, ni muhimu zaidi tukajipanga kisawasawa kabla. Hususan kwenye namna ya ushiriki wetu katika UWEKEZAJI HUO. Kwa mfano inatia aibu kwa wazawa/serikali kumiliki 20% ya hisa katika mgodi wa makaa ya mawe waliopewa Wachina. Hii ni aibu kubwa. Lazima kuwepo juhudi za kuhakikisha uchumi wetu unabaki mikononi wa watu wetu/serikali kwa kiasi walau cha 50%. Ndivyo inavyofanyika kwingineko duniani jamani!

    ReplyDelete
  2. Tutengenezeni mazingira mazuri ya utalii kwanza ndipo tuutangaze. Tusipofanya hivyo tutawaita wadhungu hapa halafu watachoshwa na huduma zetu, wakishaondoka wataeneza sifa mbaya na hatutawaona tena.

    ReplyDelete
  3. Tunapowaita wawekezaji nivizuri tuwe wazi ni kiasi gani cha umeme tunazalisha.

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...