Mwakilishi wa Kudumu wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi (kulia) akizungumza wakati wa majadiliano ya wazi ya Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa,  majadiliano  yaliyohusu Usalama na Amani Afrika;Changamoto za mapambano dhidi ya  ugaidi katika mazingira ya  kudumisha amani na usalama. Katika majadiliano hayo yaliyofanyika  Jumatatu  wiki hii,  Umoja wa Mataifa  umetahadharisha kwamba Afrika imo hatarini kugeuka kitovu  cha mashambulizi  makubwa ya kigaidi ikiwa juhudi za ziada hazitafanyika kuyakabili makundi mbalimbali ya  kigaidi kama vile Al-Shaabab,  Boko Haram na Al-Qauida


Na Mwandishi Maalum
Kama Matukio ya kigaidi yanayoendelea  kutokea   Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara na katika Ukanda wa Sahel   ya  Magharibi hayatadhibitiwa ,basi  kuna  hatari kubwa kwa  Afrika  kuwa  kitovu cha  Ugaidi na Uhalifu wa Kimataifa.
Umoja wa Mataifa, umetoa tahadhari hiyo, siku ya jumatatu wiki hii, wakati Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa chini ya Urais wa Togo lilipofanya majadiliano ya  wazi kuhusu Usalama na Amani  Afrika; changamoto za  mapambano dhidi ya  ugaidi katika mazingira ya kudumisha Amani na usalama.
Ni  katika majadiliano hayo, ambayo pia Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon alizungumza,  ilielezwa wazi  kabisa, kwamba, kama hatua madhubuti, shirikishi na endelevu hazitachukuliwa na Afrika yenyewe  na  kwa  ushirikiano  na  Jumuiya ya Kimataifa  na Taasisi mbalimbali, basi Afrika itageuka kuwa kitovu cha mashambulizi makubwa  ya kigaidi.
Makundi  ya kigaidi ambayo yanaelezwa  kujijengea himaya kuanzia  Afrika Mashariki   hadi Afrika  Magharibi ni pamoja na Al-Shabaab,Al-Qaida,  Boko  Haram  na Ansar Eddine
Karibu wazungumzaji wote waliochangia majadiliano hayo, akiwamo Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako   Manongi, licha ya kukiri kwamba vitendo vya kigaidi ni tisho kwa mustakabali wa Afrika na watu wake, lakini pia walieleza kwamba hakuna sababu yoyote inayoweza kuhalalisha vitendo vya kigaidi.
“  Hakuna sababu yoyote inayoweza kuhalilisha ugaidi” akasema  Balozi  Manongi na  kuongeza “ Ugaidi ni tishio kwa  maadili ya  ubinadamu na ni tishio kwa maendeleo na  ustawi wa nchi na watu wake”.
  Balozi Manongi, alieleza kwamba Tanzania bado inakumbuka vema matukio pacha ya kulipuliwa kwa Balozi za Marekani nchini Tanzania na Kenya mwaka1998.  Matukio ambayo Balozi wa Kudumu wa Marekani katika Umoja wa Mataifa  Susan Rice naye aliyakumbushia wakati akitoa mchango wake.
Aidha  Balozi Manongi alieleza kwamba, Tanzania pia katika siku za hivi karibuni imeshuhudia tukio  jingine la kigaidi lililotokea Mkoani Arusha.
Akaeleza kwamba  ni   kutoka na matukio hayo na hususani hili lililotokea hivi karibuni, Tanzania kupitia Kiongozi wake Mkuu, Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete, imedhamiria   kwa nvugu zake zote kuukabili  uovu huo.
 Pia alieleza mikakati mbalimbali ikiwamo ya kupitishwa kwa sheria za sera zinazolenga kudhibiti vitendo vya ugaidi na fedha haramu.
Wazungumzaji kadhaa pia walitaka kuwapo kwa juhudi   za kina za  kudadisi na kushughulikia matatizo ambayo kwa njia moja ama nyingine yanachangia kuibuka kwa makundi ya kigaidi.
Baadhi ya  matatizo hayo ni  pamoja na sababu  ukosefu wa ajira kwa vijana wengi, umaskini uliokithiri,  kutokuwapo kwa  utawala wa sheria, mbinyo wa demokrasia, machafuko ya mara kwa mara ,  na   ulinzi  hafifu  katika  mipaka  baina ya nchi na nchi.



Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

Kuna Maoni 3 mpaka sasa

  1. AnonymousMay 16, 2013

    Uelewa finyu juu ya tafsiri ya ugaidi kwa viongozi wetu utaliingiza taifa matatizoni na kutuongezea umasikini zaidi ya huu tulio nao.Leo hii unaposimama ktk majukwaa makubwa na kuinadi Tanzania kama muhanga wa matukio ya kigaidi ni hatari sana hasa ukizingatia nchi yenyewe ndio kwanza inatambaa huku ikinyosha mkono wa msaada kwa watalii,wawekezaji na wadau mbalimbali wa nje.Ni vyema kufikiri kabla ya kusema na ikibidi uzalendo utawale kwanza.

    ReplyDelete
  2. AnonymousMay 16, 2013

    Anony wa kwanza sadata mwanangu. Sio hayo tu uliyoyasema lakini naomba kuongeza kuwa unapokiri kuwa kwako ndiyo uwaja wa fujo, wajanja watakushauri waje kukulinda, ukiwaruhusu tu umekwisha!

    ReplyDelete
  3. AnonymousMay 16, 2013

    Hawa viongozi wetu wawe makini sana sio kila kitu watachoambiwa na Mataifa esp ya magharibi au na Marekani au hata hiyo so called UN kuwa ndiyo nyimbo za kuimba nchini mwao,wasome kutoka Iraq,Dunia nzima tulielezwa kwamba kuna silaha za maangamizo lazima ishughulikiwe ili dunia iwe salama baada ya maafa yote yasiosemeka wao wenyewe wanasema hakukuwa na silaha walizozitolea mpaka ushahidi UN katika baraza la usalama.Jee wanaweza KU-irreverse hiyo situation ya vita? Mataifa huwa yana intrest zao na sasa ni Afrika.










    i

    ReplyDelete

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...