Wakazi wa kijiji cha Kiwere wilayani Iringa vijijini wametoa shukrani zao za dhati kwa Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID) na kwa Chama cha Wanasheria Watetezi wa Mazingira kwa Vitendo (LEAT) kwa kuendesha mradi wa ‘Ushiriki wa wananchi katika kusimamia maliasili’.

Akiongea wakati wa tathimini ya mafunzo ya mradi, kiongozi wa kikundi cha kuhifadhi mazingira (Kiwere Hifadhi Mazingira), Hamza Chang’a alisema, kabla ya mradi alikuwa na uelewa wa kawaida kuwa ukataji miti hauruhusiwi kwa kuwa unaharibu mazingira, hakuelewa kuwa wananchi wanao wajibu wa kulinda mazingira na maliasili kwa maendeleo endelevu na kuwa jambo hilo limeelezwa katika katiba ya nchi.
“Nilipoona watu wakikata miti, niliona ni jambo la kawaida, sikufahamu athari ya muda mrefu itokanayo na vitendo hivyo, namna vianavyo athiri ubora wa maisha ya sasa na vizazi vijavyo. 
"Nilidhani ni wajibu wa kamati ya maliasili ya kijiji na viongozi wa kijiji kulinda maliasili, aliongeza.
Alisema mafunzo yamemwongeza ufahamu, yamebadilisha mtazamo kuhusu usimamizi wa maliasili, na ameanza kutumia ujuzi wake kwa vitendo kama mwananchi muwajibikaji.
Aliendelea kusema kuwa amepata dhana kamili ya ushiriki katika michakato wa maendeleo hivyo atajitolea kushawishi, kufanya kampeni na kufuatilia utekelezaji wa huduma za jamii.
Baada ya mafunzo, Chang’a na wenzake 16 waliunda kikundi cha kuhifadhi mazingira na katika kipindi cha miezi minne wamepanda zaidi ya miti 45,000 aina ya Mijoholo na Mikaratusi. Miti hiyo itapandwa katika eneo la msitu wa Msuni lilio haribiwa kutokana na ukataji miti hovyo na uchomaji mkaa.
Kwa upande wake Devotha Mihayo alisema, amejifunza kuwa uharibifu wa mazingira una athari kubwa kwa jamii hususan kwa wanawake. Unaathiri vyanzo vya maji, unasababisha ukame na njaa katika jamii. ‘Iwapo vyanzo vya maji vita haribiwa tutalazimika kutembea umbali mrefu kutafuta maji, ambapo utatupotezea muda na kuweka maisha na afya zetu hatarini’ alisisitiza.
 Kiongozi wa ‘Kiwere Hifadhi Mazingira’, Hamza Chang’a na mwanakikundi Bruno Mpagama wakionesha sehemu ya miti 45,000, waliyootesha katika bustani kijijini Kiwere

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...