RAIS wa Jamhuri ya Burundi Mhe. Pierre Nkurunziza ametembelea maonyesho ya
kwanza ya biashara ya Tanzania nchini hapa yanayolenga kuangalia soko
pana la bidhaa zinazotengenezwa na wajasiriamali kutoka Tanzania na
kusifu ubora wa bidhaa hizo.
Maonyesho hayo yaliyofanyika katika viwanja vya Tempete vilivyopo
jijini Bujumbura, yalianza Septemba 28 mwaka huu na yamekamilika leo Oktoba 1, mwaka huu yameandaliwa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara
Tanzania (TanTrade) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Bandari Tanzania
(TPA) kwa lengo la kuongeza fursa za kibiashara katika nchi za ukanda
huu wa Afrika Mashariki na Kati.
“Hii ni ishara ya kukomaa kwa udugu kati ya Tanzania na Burundi,
wananchi wa Burundi walikuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata bidhaa
hadi Dar es Salaam, lakini sasa wameletewa mlangoni.
"Kwa muda mrefu
tumekuwa tukifurahia bidhaa aina hii lakini bei zilikua kubwa kutokana
na gharama za usafiri, kwa sasa mambo yamekua mazuri,” alisema Rais
Nkurunziza.
Rais Nkurunziza aliongeza kuwa: “Uhusiano wetu unazidi kuimarika,
naaminiile dhana ya utangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki
inatekelezwa kivitendo. Naahidi kuunga mkono juhudi zote za kuimarika
kiuchumi kati ya nchi mbili hizi.”
Aidha, ubalozi wa Tanzania nchini Burundi kwa kiasi kikubwa umeshiriki
kufanikisha maonyesho haya chini ya Balozi Rajabu Gamaha ambaye ndiye
aliyewashawishi maofisa wa TanTrade kuwa na maonyesho aina hii
kutokana na maombi ya kupata bidhaa kutoka Tanzania kuwa mengi ofisini
kwake.
Awali katika hotuba yake ya ufunguzi Septemba 27 mwaka huu, Makamu wa
Pili wa Rais nchini hapa, Dkt. Joseph Bitore alisema biashara ni kitu
kinachounganisha mataifa mawili kiuchumi hivyo watachukulia maonyesho
hayo kujifunza lakini pia kutanua wigo wa mahusiano ya kiuchumi kati
ya Tanzania na Burundi.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi TanTrade, Mhandisi
Christopher Chiza alisema, uamuzi wa kupeleka bidhaa Burundi ulipofika
mezani kwake hakutaka kusita kwa sababu alijua hiyo ni njia pekee ya
kufikisha mbali bidhaa za kitanzania.
“Tunapofanikiwa kufika Burundi maana yake tunalenga soko pana la
ukanda huu, tunatarajia kufikia soko la Mashariki ya Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Kongo kwa sababu hata wao tumearifiwa kuwa wananunua
bidhaa kutoka Burundi.
“Kwa muda mrefu kama alivyoeleza mheshimiwa Rais Nkurunziza,
wajasiriamali kutoka Burundi wamekuwa wakifuata bidhaa za vyakula hasa
nafaka na mavazi kutoka pembezoni mwa mikoa ya Tanzania, lakini na wao
walikuwa wakipeleka bidhaa hizo Mashariki ya Kongo. Hivyo tunalenga
soko pana la takriban watu milioni 20, si jambo dogo.”
Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade, Bwana Edwin Rutageruka
aliahidi kuendeleza biashara kati ya Tanzania na Burundi hata baada ya
kumalizika kwa maonyesho hayo ya siku nne: “Huu ni mwanzo, tayari
wafanyabiashara tulioongozana nao wamechukua mawasiliano ya wateja wao
na watawauliza wanahitaji nini ili baadaye walete.”
Kwa muda mrefu sasa TanTrade wamekuwa katika harakati za kuondoa dhana
kuwa maonyesho ya biashara yanafanyika jijini Dar es Salaam tu, hivyo
wametanua mipaka ambapo wiki kadhaa zilizopita yalifanyika maoneyesho
makubwa ya kibiashara mkoani Kigoma na bado maonyesho mengine
yanaandaliwa katika mikoa ya pembezoni ili kuwafikia watanzania wengi
zaidi.
Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi akipatiwa maelezo kuhusu bidhaa za Tanzania kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu TanTrade, Edwin Rutageruka alipotembelea banda la Tanzania katika maonyesho ya kimataifa ya biashara yanayoendelea katika viwanja vya Tempete jijini Bujumbura mwisho mwa wiki.
Rais Pierre Nkurunziza wa Burundi akifurahia jambo kuhusu bidhaa za Tanzania alipotembelea banda la Tanzania katika maonyesho ya kimataifa ya biashara yanayoendelea katika viwanja vya Tempete jijini Bujumbura mwisho mwa wiki.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...