Na Felix Mwagara
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, amefanya ziara katika Uwanja  wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (Terminal III) ya kuvikagua vyombo vyake vinavyotarajiwa kutoa huduma katika uwanja huo hivi karibuni.
Waziri Lugola aliwasili katika uwanja huo akiwa ameambatana na Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara yake, pamoja na taasisi zake, ambapo walipokelewa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA).
Akizungumza baada ya kufanya ukaguzi uwanjani hapo, Waziri Lugola alisema hana shaka na utoaji wa huduma wa vyombo vyake katika uwanja huo mpya, kwa kuwa ameridhika na mipango ya utoaji huduma wenye weledi baada ya uwanja huo kufunguliwa.
“Wizara yangu ni wadau wakubwa katika utoaji huduma katika uwanja huu wa ndege, ni lazima nijue Jeshi la Polisi, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Idara ya Uhamiaji, wamejipangaje katika kutoa huduma bora kabisa hapa uwanjani, sina shaka nao nimeridhika baada ya kumaliza ukaguzi,” alisema Lugola.
Pia Waziri Lugola, alimuhakikishia Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Injinia Julius Ndyamukama, kuwa ameridhishwa na mpangokazi wa vikosi hivyo kwa namna viulivyojipanga kutoa huduma katika uwanja huo mpya.
“Nimeridhishwa na utendaji kazi wa Vyombo vya ulinzi na Usalama vilivyopo chini ya Wizara yangu kwa namna vilivyojipanga juu ya utendaji kazi na jinsi watakavyotoa huduma kwa wasafiri wa uwanja huu, ila nimepewa baadhi ya changamoto chache na tunaahidi kuzifanyia kazi mapema kabla ya uwanja huu kufunguliwa,” alisema Lugola.
Lugola alihakikishiwa na viongozi wa majeshi hayo kuwa, watafanya kazi kwa nguvu zote kwa kutoa huduma bora katika uwanja huo.
“Tupo tayari kuutumikia umma na kwa kuwa kazi zetu ni kuusaidia umma wa watanzania tupo tayari kuhakikisha uwanja huu mpya pamoja na viwanja vyote vinakuwa salama muda wote.”  Alisema Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt Anna Makakala.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Injinia Julius Ndyamukama, alimshukuru Waziri huyo pamoja na viongozi wa Wizara kwa kufika uwanjani hapo kufanya ukaguzi, ila alimuomba waziri huyo magari ya zimamoto yaongezwe ili kuhudumia uwanja huo mpya.
 Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto) akizungumza na Viongozi wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama (Polisi, Zimamoto na Uokoaji, Uhamiaji) vinavyofanya kazi katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), wakati alipofanya ziara ya kuvikagua vyombo vyake vitakavyotoa huduma uwanjani katika uwanja mpya wa Terminal III unaotarajiwa kufunguliwa hivi karibuni.
 Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, akimuuliza swali Mkurugenzi wa Viwanja vya Ndege, Paulo Rwegasha (watatu kushoto), wakati alipofanya ziara katika Uwanja wa Ndege cha Julius Nyerere (JNIA-Termila III) kwa ajili ya kuvikagua vyombo vyake vitakavyotoa huduma katika Uwanja huo unaotarajiwa kufunguliwa hivi karibuni.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Jacob Kingu, akizungumza katika kikao kabla ya kumkaribisha Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, (wapili kulia), kuzungumza na maafisa wa Jeshi la Polisi, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na Idara ya Uhamiaji ambao watatoa huduma katika Uwanja mpya wa Ndege wa Julius Nyerere Terminal III unaotarajiwa kufunguliwa hivi karibuni.
 Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala, akimfafanulia jambo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola (kushoto), na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali Jacob Kingu, katika moja ya ofisi zitakazotumiwa na Maafisa wa Uhamiaji kwa ajili ya ukaguzi wa wasafiri watakaotumia Uwanja mpya wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, unaotarajiwa kutumika hivi karibuni.
 Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), Injinia Julius Ndyamukama akimfafanulia jambo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, (wapili kushoto), Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali, Jacob Kingu (watatu kushoto), na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Ramadhan kailima (kushoto), wakati Waziri huyo alipofanya ziara Uwanja mpya wa  Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) kwa ajili ya kuvikagua vyombo vyake ambayo ni Jeshi la Polisi, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Idara ya Uhamiaji vinavyotarajiwa kutoa huduma hivi karibuni.

Msimamizi wa Mradi kutoka Wakala wa Ujenzi (Tanroad) Burton Komba akimwelekeza Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, (aliyeshika kitabu), sehemu mbalimbali za Uwanja mpya wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, wakati Waziri huyo alipofanya ziara ya kuvikagua vyombo vyake ambayo ni Jeshi la Polisi, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Idara ya Uhamiaji vinavyotarajiwa kutoa huduma hivi karibuni. Wapili kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali, Jacob Kingu, na kulia ni Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Makakala. (Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi)

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...