Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), yashiriki maonesho ya 27 ya wakulima, wavuvi na wafugaji yanayoadhimishwa kitaifa katika viwanja vya Nyakabindi, wilayani Bariadi mkoani Simiyu. 

Maonesho hayo yenye kauli mbiu ‘Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa Ukuaji wa Uchumi wa Nchi’ yamelenga kutoa fursa kwa taasisi mbalimbali nchini za serikali na binafsi kutoa elimu hasa ya teknolojia wanazozitumia na namna zinavyoweza kuwasaidia wakulima katika kurahisisha utekelezaji wa majuku yao ya kila siku ya kilimo, ufugaji na uvuvi.
Meneja Usajili wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa Bi. Julien Mafuru ameeleza kuwa NIDA imeshiriki kwenye maonesho ya Nanenane mwaka huu ili kutoa fursa kwa wakulima, wafugaji na wavuvi Kusajiliwa kwa ambao hawajawahi Kujitokeza Kusajiliwa popote nchini, waombaji kuangalia taarifa za maombi ya Usajili yalikofiki kwa waliokamilisha Usajili, Elimu juu ya namna ya kupata Nakala ya Kitambulisho cha Taifa kupitia tovuti ya NIDA ( www.nida.go.tz ), Matumizi ya Namba ya Utambulisho (NIN) na Kitambulisho cha Taifa, kukusanya maoni ya wateja kwa lengo la kupata mrejesho juu ya huduma zetu, kutangaza njia zetu mbalimbali tunazotumia kuwasiliana na wananchi pamoja na kutangaza ofisi zetu za Usajili zilizopo katika kila wilaya nchini.

Bi. Mafuru ameeleza kuwa mwitiko wa wananchi ni mkubwa hasa kundi la watu ambao waliokamilisha Usajili siku za nyuma, wengi wamefika katika banda la NIDA Na. 7 kwenye viwanja vya Nyakabindi na kupatiwa namba zao za Utambulisho wa Utaifa (NIN) kwa ambao zimeshatoka. Namba hizo zimewasaidia kutambulika na kuweza kufika pia katika mabanda ya wadau wetu walioko katika maonesho haya ili kupata huduma nyingine za kijamii na kiuchumi kama vile kusajili laini, kukata TIN, kufungua akaunti ya benki, kupata mkopo kwenye SACCOSS n.k.
Kwa Upande wake Bi Fatuma Odoyo, mwananchi mkazi wa Bariadi ameishukuru serikali ya awamu ya 5 kupitia NIDA kwa kusogeza huduma karibu na wananchi kupitia kutoa huduma za Usajili kwenye maonesho ya Nanenane kwani alikuwa bado hajafika kwenye ofisi za Usajili za NIDA kupata huduma hiyo. 

’Ndani ya maonesho haya niliposikia matangazo kwenye redio kuwa NIDA wapo nikafika kwenye banda lao na kuanza Kujisajili kwani nahofia laini yangu ya simu kufungwa muda wa ukomo ukifika wa kutakiwa kusajili laini ya simu kwa kutumia alama za kibaiolojia ambapo wanatuhitaji tuwe na namba ya NIDA’ Bi Fatuma amesema.
 Mmoja wa wananchi wa Mkoa wa Simiyu aliyejitokeza kujiandikisha ili kupata Kitambulisho cha Taifa akijaza fomu ya usajili.

Bi Careen Kuwite Afisa Msajili Mkoa wa Simiyu ameeleza kuwa wananchi hususan kundi la wakulima, wavuvi na wafugaji wanapotambuliwa katika mfumo wa Utambuzi unaosimamiwa na NIDA na kupatiwa Namba ya Utambulisho, kunawawezesha kupata huduma za kijamii kirahisi kama vile kupata ruzuku za pembejeo za kilimo, kusajili laini ya simu, kujisajili kwenye vyama vya ushirika (kwa wakulima, wavuvi na wafugaji), kufungua akauti ya benki, kupata msaada wa TASAF unaotolewa kwa kaya masikini, hati miliki ya kiwanja na nyumba, hati ya kusafiria ya kielekroniki, kusajili biashara na kampuni brela, kukata leseni ya udereva, kukopesheka kirahisi kwenye taasisi za fedha, kupata mkopo wa elimu ya juu kwa wanafunzi, kuomba ajira, malipo ya pensheni pamoja na huduma nyingine nyingi.
Baadhi ya Wananchi wa Mkoa wa Simiyu wakiendelea kupatiwa huduma ya kujisajili ili wapate vitambulisho vya taifa, walipotembelea banda ya NIDA katika maonyesho ya Nane Nane yanayoendelea katika uwanja wa Nyakabindi, Bariadi mkoani Simiyu leo.

Akihitimisha Bi. Julien amewasihi wakulima, wavuvi, wafugaji na wananchi wote kiujumla kujitokeza Kusajiliwa kwa wingi ili kupata Namba ya Kitambulisho cha Taifa kwa wakati. 

Aidha ameeleza kuwa wananchi watakaoshindwa kutumia fursa ya Kusajiliwa kwenye maonesho haya ya 27 ya Nanenane wafike kupata huduma katika ofisi za Usajili za NIDA zilizoko katika kila wilaya nchi nzima wakiwa wamekamilisha kujaza fomu za Usajili zinazopatikana serikali za mitaa, kwenye tovti ya NIDA na kwenye ofisi za Usajili za NIDA.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...