VIWANDA vya ndani nchini vimepongezwa kwa kuwa na uwezo wa kuongeza thamani ya korosho ya Tanzania tangu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli alipotangaza uamuzi wa Serikali kununua korosho zote za wakulima tarehe 12 Novemba, mwaka 2018.

Taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Habari na Mawasiliano Wizara ya Viwanda na Biashara imesema kuwa hayo yamesemwa leo Oktoba Mosi na Prof. Joseph Buchweishaija, Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara alipofanya ziara ya kufuatilia ubanguaji wa korosho kwenye viwanda vilivyopo Mikoa ya Mtwara na Lindi na usafirishaji wa korosho hizo nje ya nchi unaoendelea katika bandari ya Mtwara.

“Nimejionea mwenyewe korosho zetu zilivyo na ubora unaostahiki, zinabanguliwa kwa utaalam na zimefungashwa kwa kutumia vifungashio vizuri (vacuumed packed) katika madaraja yote hususan daraja la WS320 linalopendwa na wanunuaji wengi kutoka nje ya nchi. Hakika viwanda vyetu vinafanya kazi nzuri “amesema Prof. Buchweishaija.

Prof. Buchweishaija amesema kuwa ubanguaji wa korosho uligawanyika kwa viwanda vya aina mbili yaani viwanda vidogo vinavyosimamiwa na SIDO pamoja na viwanda vikubwa.

Amesema katika kutekeleza mpango wa ubanguaji, Serikali kupitia Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko (CPB) iliingia mikataba na viwanda vikubwa pamoja na Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) kwa niaba ya viwanda/wabanguaji wadogo ili kubangua korosho. Kwa viwanda vidogo kwa Mkoa wa Mtwara vilikuwa vitano ambavyo ni Siwa Food Products, Mama Vitu Super Cashewnut, Mikindani Food Processing, Akross Ltd - SIDO, Mtwara na Kitama Farmers- Tandahimba na kwa Mkoa wa Lindi vilikuwa viwanda vitatu ambavyo ni Waigero Ltd, Wabanguaji Wadogo BUCO, na Uwakoru, Ruangwa. 

"Hadi sasa viwanda vitano vilivyochini ya usimamizi wa SIDO Mtwara ambavyo vimekamilisha ubanguaji wa korosho na viwanda viwili ambavyo ni Waigero na Uwakoru chini ya usimamizi wa SIDO Lindi vinaendelea na uzalishaji na ubanguaji. Hadi kufikia Septemba 23 mwaka 2019 Korosho tani 607.75 zimebanguliwa na viwanda vyetu vidogo na kuwezesha wabanguaji wadogo takribani 1,000 kupata ajira. 

Kwa upande wa viwanda vikubwa Serikali iliingia mikataba na viwanda sita (6) ambavyo ni Amama Framers kilichopo Tandahimba, Perfect Cashew kilichopo Masasi, Hawte Investment kilichopo Mtwara, Al-Andalus kilichopo Lindi, Micronix kilichopo Masasi na Korosho Afrika kilichopo Tunduru. Hadi kufikia Septemba 23, 2019 Korosho tani 3,309.64 zimebanguliwa na viwanda vikubwa na viwezezesha kutoa ajira takribani 2,511 ambao kwa asilimia kubwa ni akina mama. Hadi kufikia Septemba 23,mwaka 2019 viwanda vinne ambavyo ni Amama Farmers, Perfect Cashew, Hawte Investment Ltd na Al-Andalus Ltd vinaendelea na ubanguaji wakati Kiwanda cha Micronix na Korosho Afrika vimemaliza ubanguaji wa korosho ghafi kama makubaliano ya mkataba yao ambapo kwa sasa viwanda hivyo viwili vinaendelea kubangua korosho zao walizouziwa na Serikali kiasi cha tani 1,000.

Kwa upande wa usafirishaji wa korosho kutoka kwenye Ghala mbalimbali kwenda melini, zoezi linaendelea vizuri.Ameongeza kuwa hadi Septemba 23 mwaka 2019 Korosho takribani tani 40,050 zimeshapakiwa kwenye meli tayari kwenda nje ya nchi kupitia bandari ya Mtwara.

“Hivi sasa ninavyozungumza tayari meli mbili zimepakia korosho na kuondoka, meli ya tatu imeanza kupakiwa ambapo itabeba kontena 1015 ambazo sawa na tani 23,328 na zoezi zima litakamilika kwa siku mbili ukizingatia kuwa kuna meli zingine mbili zipo majini na zitatia nanga na kuanza zoezi la kupakia korosho kwenda nje ya nchi” ameeleza Prof. Buchweishaija.

Ameweka wazi kuwa ubanguaji wa korosho zilizonunuliwa na Serikali zimeweza kutoa ajira hasa kwa wanawake kwa asilimia 92, hivyo wamefanikiwa vizuri na kuonesha dalili kuwa Tanzania inaweza hasa wanapozungumzia nchi ya viwanda maana tukiuza korosho ghafi tunahamisha ajira huku akitoa mwito kwa viwanda kuendelea kuongeza uzalishaji ili ikiwezekana korosho zote zinazozalishwa Tanzania zibanguliwe nchini.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...