Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Mhe Freeman Mbowe (Mb), ametoa ombi maalum kwa Mtume na Nabii Josephat Mwingira  kuungana na Viongozi wengine wa kiroho kutoka dini zote kuliombea taifa katika mwaka huu wa Uchaguzi Mkuu.

Mhe. Mbowe ameyasema hayo kwenye ibada maalum ya kuombea na kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa baba wa Nabii na Mtume wa Kanisa  la Huduma ya Efatha, Josephat Mwingira, Mzee Elias Mwingira, leo Jumamosi 22 Februari 2020, Kwa Mathias, Kibaha mkoani Pwani.

"Ombi langu maalum kwako Nabii na Mtume Josephat Mwingira, wewe na viongozi wengine kutoka dini zote, mkaungane kuliombea taifa katika mwaka huu wa uchaguzi" Mhe. Mbowe.

"Pia mkatuombee sisi  Viongozi wa kisiasa tuache viburi, tuvae unyenyekevu, tukawe na tume huru ya uchaguzi katika uchaguzi ujao, haki ikatamalaki" ameongeza Mbowe.

Akitoa salamu za pole, Katibu Mkuu wa Chadema, Mhe John Mnyika (Mb), pia ametaka watumishi wa Mungu waliombee taifa letu, ili haki iweze kutamalaki, kwani haki huinua taifa.

 "Tuitumie siku hii ambayo tunasherekea maisha ya baba yetu, Elias Mwingira, ikawe pia faraja kwa familia,  naomba watumishi na kanisa, tuliombee taifa haki ikatendeke, kwani haki huinua taifa, Mzaburi Daudi katika Zaburi 15 anasema Mtu atendae haki hataondoshwa milele" Mnyika.

Mbunge wa Kawe, Mhe Halima Mdee ambae ni Mbunge wa jimbo analoishi Nabii na Mtume Josephat Mwingira , amesema baada ya kusikiliza historia ya Mzee Elias Mwingira, jinsi alivyomlea mtoto wake, amejifunza mengi na kutaka wazazi wa sasa wa kigigitali, mtoto anapokosea apewe anachostahili.

 "Sisi Wakatoliki katika amri za Mungu katika ile amri ya 5, inasema Muheshimu baba yako na mama yako ili siku zako ziwe nyingi katika nchi upewayo na baba Mungu wako, Elias Mwingira aliwaheshimu wazazi wake, ndio maana ameishi maisha marefu, miaka 94+ sio shughuli ndogo" amesema Halima Mdee (Mb).

Pia akizungumza katika ibada hiyo, Waziri Mstaafu na Mwenyekiti wa Chadema kanda ya kati, Mhe. Lazaro Nyalandu, amesema Mungu aliweka kitu kwa Mzee Elias Mwingira, anaesherekewa maisha yake leo, akakihamishia kwa Nabii na Mtume Josephat Mwingira.

"Tunaposherekea maisha ya Mzee Elias Mwingira, wewe Nabii na Mtume Mwingira, Mungu akakufanye kuwa taifa kubwa, kupitia kwako, Mungu akafunuliwe, Tanzania, Afrika na dunia nzima" amesema Mhe. Nyalandu.

"Kupitia Efatha Ministry ule upendo wa zamani enzi za Nyerere ukaonekane, haki ikatamalaki, duniani tunaishi miaka 100+ na baadae ufalme wa mbinguni" ameongeza  Mh. Nyalandu.

Akitoa neno la shukrani kwa waombolezaji ambao leo wameitwa washerekeaji Nabii na Mtume Josephat Mwingira amesema "Washindi huja hapa, washindi wamekuja hapa, walioshindwa hawajafika ,hapa wanakuja washindi"  Nabii na Mtume Josephat Mwingira.

Akaongeza "Mhe. Mbowe umeminywa sana, lakini nime-observe wewe ni mvumilivu sana, mvumilivu hula mbivu, subiri mbivu zako" Nabii na Mtume Josephat Mwingira.

 Viongozi wengine waliohudhuria ibada hiyo ya kusherekea maisha ya Mzee Elias Mwingira, ni Naibu Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Tulia Ackson, Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, Mhe. James Mbatia, Meya wa Ubungo, Mhe Boniface Jacob na Mkuu wa Mkoa Mstaafu Mhe Nikodemus Banduka.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...