*Aanika mipango yake ya kuwatumikia wananchi wa Ubungo kwa miaka mitano ijayo

*Asisitiza umoja na mshikamano, awataka watanzania kujiepusha na vurugu 

Na Said Mwishehe,Michuzi TV

RAIS wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania ambaye pia ni Mgombea urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi(CCM)katika Uchaguzi Mkuu mwaka huu, Dk.John Magufuli ameagiza kuanzia leo Soko la Ndizi Mabibo maarufu Mahakama ya ndizi lililopo jijini Dar es Salaam liwe chini ya wananchi na kwamba wasisumbuliwe na mtu yoyote.

Dk.Magufuli ametoa maagizo hayo leo mbele ya maelfu ya wananchi wa Wilaya hiyo Ubungo waliofika kumsikiliza licha mvua kubwa kunyesha na kusababisha kuwaambia kwa jinsi ambavyo wamejitokeza kwa wingi huo yuko tayari kuwasikiliza kero inayowasumbua.

"Niko tayari kusikiliza kero mojawapo ya hapa, nasikia pale Mahakama ya ndizi kuna kero ambayo inawasumbua.Mahakama ya ndizi mnataka nifanye nini? Wana mateso gani?

"Kwa heshima ambayo mmenionesha nataka kuwaeleza wananchi kwa mamlaka niliyonayo soko hili sasa litabakii chini ya wananchi wa hapo ambao waendelee kufanya biashara, kama kutakuwa na sheria nyingine za  Wizara ya Ardhi na Sheria zote ambazo ziko chini ya Rais kuanzia hapo patakuwa chini yao na hawatalipa ushuru bali watalipia kitambulisho mabacho cha 20,000 na asitokee mtu wa kuwasumbua,"amesema Dk.Magufuli.

Kabla ya kutoa maagizo hayo  Rais Magufuli alimuita mgombea ubunge jimbo la Ubungo Profesa Kitila Mkumbo ili kuelezea kero iliyopo katika soko hilo la Mahakama ya ndizi ambapo alifafanua soko hilo linashindwa kuendelezwa kwani kuna mgogoro wa umiliki kati ya wananchi na kiwanda cha Urafiki.

Baada ya maelezo hayo ndipo Dk.Magufuli akatangaza rasmi soko hilo limerudi kwa wananchi kuanzia leo hii Oktoba 13 mwaka huu, na mambo ya kiseria yashughulikiwe haraka.

Pamoja na maagizo hayo,Dk.Magufuli ametumia nafasi hiyo kuwaeleza wananchi hao mikakati aliyonayo katika kuwatumikia kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.

Ambapo amesema kwamba mwaka 2915 alifika mbele ya wananchi hao kuomba kura."Nilikuka kuomba kura, mimi mnilinipa lakini kwa wabunge mkaninyima,hivyo nilikuwa na wakati mgumu wa kuleta maendeleo.Maendeleo ambayo tumefanya ni kwa tabu sana.Nafahamu hata hapa Mburahati kuna barabara za lami.

"Na miradi hii ambayo tunaifanua ni ya kitaifa, lakini hapa imekwama kwasababu ya kuwa na wapinzani, na ndio maana hata safari hii aliyekuwa mbunge wa Kibamba na Ubungo wameshindwa hata kugombea tena maana wanajua waliwakosea wananchi 

"Naomba mchague wagombea wa CCM , na nasema hivyo sio kwasababu nawachukia wapinzani,  hapana .Siwachukii na maendeleo hayana vyama lakini maendeleo ya kweli yataletwa na CCM,"amesema Dk.Magufuli.

Ameeleza jinsi ambavyo Wilaya ya Ubungo imepiga hatua kubwa kimaendeleo katika sekta mbalimbali."Tumefanya mambo makubwa ya maendeleo na niwahakikishie tutaendelea kufanya maendeleo makubwa zaidi kwa wananchi hawa wa Ubungo na Kibamba."

Kuhusu maji Dk.Magufuli amesema katika Jiji la Dar es Salaam, Serikali katika miaka mitano imeweka mkazo katika kutatua changamoto ya uhaba wa maji na sasa maji yanapatikana maeneo mengi ya jiji hilo.

"Leo hii hata mikokoteni ya kuuza maj imepungua mtaani, magari ya kubeba maji leo hii yanatangatanga hayana pakwenda.Nilimchagua Profesa Kitila Mkumbo kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na amefanya kazi kubwa sana katika kutatua changamoto ya maji Ubungo,Kibamba na maeneo mengine ya Jiji la Dar es Slaam.

"Nasikia kuna watu wanasema kuhusu ukabila wanasema Kitila Mkumbo ni wa Singida.Tuache mambo ya ukabila ambao Mwalimu Nyerere aliumaliza , tuache kuleta ukabila. Hapa katika mkutano wapo wa makabila yote na dini zote, na ndio Tanzania yetu ilivyo,"amesema Dk.Magufuli.

Ametumia nafasi hiyo kufafanua Wilaya ya Ubungo na Kibamba pamoja na kuwepo kwa barabara za lami,bado kunachangamoto ya barabara za lami katika mitaa kwa kutokuwa na lami, ameomba apelekewe wagombea hao wa wa majimbo hayo ili afanye kazi ya kujenga barabara hizo na wabunge wa Chama hicho watapendekeza barabara ambazo wanataka ziwekewe lami na yeye atatekeleza.

Wakati huo huo, Dk.Magufuli amesema Wilaya ya Ubungo haina majengo ya halmashauri na hivyo akichaguliwa tena kuongoza nchi atasimamia kuhakikisha Ubungo wanakuwa na jeng lao kama ilivyo Wilaya mpya ya Kigamboni ambayo yenyewe ilishajenga jengo lake.

"Wilaya ya Kigamboni ni mpya lakini tayari ina majengo yake ya halmashauri , wamepata haraka kwasababu walikuwa na wabunge wa CCM na hivyo ilikuwa rahisi kufanikisha mipango yao ya maendeleo,"amesema Dk.Magufuli.

Kuhusu ujenzi wa miundombinu, Dk.Magufuli amesema kwamba wapinzani wamekuwa wakisema daraja la Ubungo waliomba wao, jambo ambalo sio kweli na ni uongo wa mchana kweupe kwani daraja hilo na mengine yamejengwa na Serikali ya CCM kwa kutambua umuhimu wake na hasa ya kuondoa foleni katika majimbo ya Ubungo na Kibamba na maeneo mengine ya Dar es Salaam na wamefanya hivyo  kwa faida ya watanzania wote .

Dk.Magufuli amesema ili kuleta maendeleo katika jimbo la Ubungo na Kibamba amewaomba wananchi kuhakikisha wanamchagua Profesa Mkumbo na Jumanne Mtemvu wa jimbo la Kibamba ili walete maendeleo ya wananchi."Naomba mniletee hawa vijana wawili, nileteeni wagombea udiwani wa majimbo ya Ubungo na Kibamba ,tulete maendeleo.

"Nchi yetu imeibiwa vya kutosha, tumewabana na wakubwa wamenuna,wamekasirika ,hivyo wameamua kutumia vibaraka ili watutoe madarakani,"amesema Dk.Magufuli na kuwataka Watanzania kuungana katika kuleta maendeleo bila kujali vyama vyao.

Pamoja na hayo,Dk.Magufuli amesema siasa isitumike kama kichaka cha kuwagombanisha Watanzania, kwani wanaotaka kuvuruga nchi wao mambo yakiharibika watakimbia,hawatakaa hapa."Watakachokifanya ni kuchocheaa weee halafu wao watakimbia.Msikubali kuiharibu nchi yetu,msiwape kura.

"Nchi yetu ikisambaratika maadui watatumia nafasi hiyo kuiba rasilimali zetu .Watanzania naomba niwaambie nchi yetu Tanzania, tumezaliwa Tanzania, tunaishi Tanzania na tutazikwa Tanzania,hatuna nchi nyingine ya kwenda zaidi ya hii.Tuitunze na hao ambao wanataka kutugawa na kuharibu amani ya nchi msiwachague katika uchaguzi mkuu mwaka huu,"amesema Dk.Magufuli.


Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...