Na Muhidin Amri,Mbinga
WAZIRI wa madini Dotto Biteko, ametembelea mgodi wa dhahabu wa Lukalasi 
 katika wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma unaomilikiwa na mzawa Jonson 
Nchimbi na kupongeza kazi nzuri inayofanywa na mwekezaji huyo.
Waziri Biteko amesema, wizara ya madini itaendelea kumuunga mkono 
mwekezaji huyo mzawa katika shughuli za utafutaji na uchimbaji wa 
madini.
Kwa mujibu wa Waziri Biteko,  katika kipindi kifupi mwekezaji huyo  
amechimba dhahabu yenye thamani ya zaidi ya Sh Bilioni 3 na amelipa  
zaidi ya Sh milioni 200 kama kodi kwa Serikali.
Amewaomba wananchi wanaofanya kazi katika mgodi huo kufanya kazi kwa 
uaminifu  na kujiepusha na vitendo vya wizi vinavyoweza kumvunja moyo 
mwekezaji huyo mzaliwa wa mkoa wa Ruvuma.
Amesema, haya madini ni nyenzo pekee ambaye Watanzania tumepewa na Mungu
 ili tuondoa umaskini wetu,kwa hiyo ni lazima tuchimbe kwa haki,kulipa 
kodi na kufuata sheria na taratibu za nchi badala ya kutugombanisha.
Waziri Biteko amesema,kwa kutambua uwekezaji huo, Serikali itaendelea 
kumsaidia kwa kumpatia wataalam ili aweze kuchimba dhahabu kisasa na 
kumkutanisha na taasisi mbalimbali za fedha ili  kupata mikopo.
Amesema, lengo  ni kumwezesha kupata vifaa vya kisasa kwa ajili ya 
shughuli za uchimbaji wa madini kwa  sababu bado ana vifaa vya kizamani.
Amesema, serikali  inatambua leseni zote na baadhi bado hazijafanyiwa 
kazi na nyingine zimeisha muda wake, hivyo wizara ya madini itazifuta 
ili kupewa watu wengine watakaokuwa tayari kuchimba na kuachana na watu 
wenye tabia ya kushikilia maeneo bila ya kuyafanyia kazi.
Amesema,uchimbaji  wa madini ni safari ndefu na serikali inawahitaji 
sana wachimbaji wakubwa na wadogo  na kamwe wizara haitaruhusu kuwepo 
kwa wachimbaji wakubwa pekee yake kwani inahitaji watu wengi kufanya 
utafiti ili kufahamu kiasi cha madini kilichopo katika nchi yetu.
Ameiagiza,ofisi ya Mkuu  wa Ruvuma na mkuu wa wilaya Mbinga kuhakikisha 
inapitia upya maeneo na leseni zote ambazo hazijaendelezwa ili maeneo 
hayo yaweze kupewa vikundi vidogo kwa ajili ya uchimbaji.
Mmiliki wa mgodi huo Jonson Nchimbi amesema,tangu mgodi ulipoanzishwa 
wameweza kuzalisha dhahabu yenye thamani ya Sh.bilioni 3,038,167,518.24 
na kulipa mrabaha wa Sh.182,290,051.09,ada ya ukaguzi Sh. Milioni 
30,381,675.18 pamoja na ushuru wa Halmashauri jumla ya Sh.9,114502.55.
Aidha amesema,mgodi  unashiriki  shughuli mbalimbali za kijamii na  za 
maendeleo katika kijiji cha Lukalasi na umetoa ajira kwa wananchi 
wasiopungua 300 wanaofanya kazi mbalimbali ikiwa ni pamoja na uchimbaji 
wa dhahabu juu ya ardhi.
Hata hivyo amesema, kwa kuwa eneo hilo limeanza kujulikana kuwa na 
uzalishaji mzuri wa dhahabu kumeanza kutokea migogoro michache ya 
kuingiliana katika  leseni za uchimbaji na kuishukuru wizara ya madini 
kumaliza moja kati ya migogoro hiyo.
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Balozi Wilbert Ibuge amesema,serikali inatambua 
uwezo wa mgodi huo katika kuongeza ajira na mapato ya serikali na mapato
 binafsi.
Balozi Ibuge,amewataka wananchi wanaishi kuzunguka mgodi huo kutambua 
juhudi za uwekezaji  na kazi inayofanyika  katika mgodi huo ambao tangu 
ulipoanzishwa umeshaleta manufaa makubwa.
Hata hivyo,ametaka kufanyiwa kazi tatizo la  kushuka kwa uzalishaji wa 
dhahabu katika mkoa huo ambapo kwa Mwezi Julai dhahabu iliyopatikana ni 
kilo  2,wakati mwezi Juni ilikuwa kilo 4, na Mwezi Mei kilo 5.
Amesema, serikali ya mkoa itaendelea kuunda vikundi vingi na kuwataka 
viongozi wa chama cha wachimbaji madini mkoa wa Ruvuma kuhamasisha 
wanachama wake kwa kuwa lengo la Serikali ya mkoa ni kutoa ajira na 
kuongeza mapato yatokanayo na madini.
Waziri wa Madini Dotto Biteko kushoto na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Balozi Wilbert Ibuge kulia,wakimsikiliza jana mmiliki wa mgodi wa dhahabu Lukalasi wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Jonson Nchimbi katikati wakati wa ziara ya Waziri wa madini alipotembelea mgodi huo ili kujionea kazi zinafanywa na mwekezaji huyo.,Mmiliki wa mgodi wa dhahabu Lukalasi katika wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Jonson Nchimbi kulia,akitoa taarifa ya hali ya uzalishaji wa dhahabu kwa Waziri wa Madini Dotto Biteko katikati, aliyetembelea mgodi huo akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Ruvuma,kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Balozi Wilbert Ibuge.
Picha na Muhidin Amri,


 
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...