MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango akiambatana na mkewe mama Mbonimpaye Mpango leo tarehe 24 Januari 2022 wamemtembelea na kumpa pole Makamu wa Rais mstaafu Dkt Mohammed Gharib Bilal kufuatia kifo cha mama yake mzazi Bi. Safia Abeid kilichotokea tarehe 3 Januari 2022 na kuzikwa kijijini kwao Kaboje Wilaya ya kati Mkoa wa Kusini Unguja tarehe 4 Januari 2022.
Makamu wa Rais Dkt. Mpango amewapa pole wanafamilia na kuwaomba kuendelea kumuombea marehemu ili apumzike kwa Amani. Kwa upande wake Makamu wa Rais mstaafu Dkt. Bilal amemshukuru Makamu wa Rais kwa kuwapa faraja wanafamilia kufuatia msiba huo. Wakati huo huo Makamu wa Rais mstaafu Dkt Bilal amempa pole Dkt. Mpango kufuatia kifo cha kaka yake Askofu Mstaafu Dkt. Gerald Mpango kilichotokea tarehe 19 Januari 2022.
Katika hatua nyingine Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango ameitembelea na kutoa pole kwa familia ya mwanasiasa mkongwe mzee John Alfonso Nchimbi aliyefariki jumapili tarehe 23 Januari 2022 katika hospitali ya JKCI Jijini Dar es salaam.
Akiwa Tabata nyumbani kwa marehemu, Makamu wa Rais amempa pole mke wa marehemu Bi. Selva Nchimbi ,mtoto wa marehemu Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi pamoja na ndugu, jamaa na marafiki waliojitokeza katika msiba huo. Makamu wa Rais amewaomba wanafamilia pamoja na waombolezaji kuwa na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu na kuendelea kumuombea marehemu mzee John Nchimbi apumzike kwa Amani.
Mazishi ya mwanasiasa mkongwe mzee John Nchimbi yanatarajiwa kufanyika jumanne tarehe 25 Januari 2022 katika makaburi ya Kinondoni jijini Dar es salaam.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...