Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV

MCHEZAJI wa Kimataifa wa Ghana, Bernard Morrison ameomba msamaha Mashabiki wa Yanga SC kwa kitendo cha kuondoka Klabuni hapo, miaka miwili iliyopita na kuhamia kwa Watani wa Jadi Simba SC, uhamisho ulioleta utata kwenye mkataba.


Morrison ameomba radhi mbele ya Mashabiki lukuki wa timu hiyo na Uongozi wa Klabu hiyo wakati akitambulishwa katika tamasha la Siku ya Mwananchi kwenye dimba la Benjamin Mkapa, Dar es Salaam, Agosti 6, 2022.


“Naomba msamaha kwa Mashabiki wote wa Yanga S.C. kwa miaka miwili iliyopita kuondoka klabuni hapa, najua hamkufurahi lakini nimerudi na nawaomba msamaha, bado naipenda Yanga S.C.”, amesema Morrison.


“Miaka miwili iliyopita, niliwahi kupanda kwenye jukwaa hili nilisema nipo kwenye Chuo Kikuu cha Soka la Tanzania na kwa sasa kwenye Klabu ya Yanga nipo kwenye ‘level’ nyingine ya Shahada ya Pili (Master’s Degree)”, amesema Morrison.


Pia, Morrison amesema wanaamini kufanya vizuri msimu ujao kutetea mataji yote matatu ambayo wametwaa msimu uliopita, mataji ya Ligi Kuu Soka Tanzania Bara, Michuano ya ASFC, na Ngao ya Hisani.


Morrison amesema, “Kwa sasa Yanga S.C. imekuwa kubwa sana imesajili Wachezaji wazuri wenye viwango na kuna Kocha Mkuu, Nasreddine Nabi ambaye amefanikisha yote msimu uliopita akishirikiana na Benchi lake la Ufundi”.


Kwenye tamasha hilo, Msemaji wa Klabu hiyo, Haji Sunday Manara amefanya ‘surprise’ kwenye tamasha hilo la Wananchi baada ya kudai kufika kama ‘MC’ aliyealikwa kwenye shughuli hiyo ambayo imehudhuriwa na idadi kubwa ya Mashabiki.


“Mimi nimekuja kama walivyokuja kina Maulid Kitenge, Zembwela na Dacota, mimi nimealikwa tu kama ‘MC’ na nikitoka hapa naenda kwenye shughuli huko Kigogo, ahsanteni sana Wananchi”, amedai Manara.
 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...