Ashrack Miraji same kilimanjaro

KATIBU Tawala Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro (DAS),Upendo Wella amebainisha kuwa changamoto ya wanyamapori  hasa tembo kuvamia  jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi wilayani hapo  umepatiwa ufumbuzi wa kudumu ambao utekelezaji wake utaanza hivi karibuni.

Hayo ameyasema alipokuwa mgeni rasmi akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Same Kasilda  Mgeni kwenye  uzinduzi wa ofisi ya Shirika la Kimataifa la Utunzaji Mazingira (WWF) Kanda ya Mkomazi Wilayani Same.

Wella amesema serikali kwa kushirikiana na mashirika ya uhifadhi nchini  wamedhamiria kumaliza kero ya wanyamapori (tembo) ambao wamekuwa wakivamia makazi ya binadamu na kufanya uharibifu kwa sababu ya kutafuta maji.

Amesema moja ya hatua ya kutatua changamoto hiyo ni  mpango madhubuti wa kuchimba visima katika maeneo ya hifadhi  kuhakikisha wanyamapori  hawatoki kwenda kufanya uharibifu kwenye makazi ya watu walio maeneo ya karibu na hifadhi

"Tutoe elimu lakini pia tuweke mikakati ya kuweka visima kule hifadhini kuhakikisha hawa wanyama hawatoki nje,kiukweli sote ni mashuhuda,mvua mara baada ya kunyesha,changamoto ya tembo mimi sijaisikia" amesema Wella.

Kwa upande wake Meneja Mradi wa Shirika la  WWF,Novati Kessy ametaja moja ya hatua nyingine ya kutatua mgogoro huo ni kutoa elimu ya kujilinda  pamoja na kupeleka askari wa hifadhi  kwenye vijiji vinavyoathiriwa na adha hiyo ili  kuimarisha  doria na kudhibiti wanyamapori wasifanye uharibifu.

Wakati huo huo ofisa wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania ikolojia ya Mkomazi (TAWA),Juma Kibona amesema wameandaa andiko litakalo wawezesha kuchimba mabwawa katika hifadhi ya Mkomazi ambapo  wanyama watapata  maji jambo amabalo amesema ndilo litakuwa mwarobaini wa kudumu wa kero hiyo.

Awali Mwenyekiti wa Chama Cha Wafugaji Tanzania Kanda ya kaskazini (CCWT) ,Lekey Laizer amesema  licha ya tembo kuathiri jamii yao hawana budi kushirikiana na mashirika hayo ya uhifadhi nchini kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu kwa sababu ulinzi ni jukumu lao wote.





Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...