📌 Shilingi bilioni 43.9 kusambaza umeme kwenye vitongoji 379
📌 Kampuni ya Giza Cable kuanza kazi ya kusambaza umeme vitongoji vya mkoa wa Dodoma
📌 Wananchi zaidi ya 12,000 kufikishiwa huduma hiyo
Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule ametoa wito kwa Wananchi wa vitongoji vitakavyonufaika na Mradi wa Kusambaza Umeme katika vitongoji 379 kujiandaa kwa kutandaza nyaya majumbani (Wiring) mapema ili kuunganishwa na huduma hiyo mara Mradi utakapokamilika.
Akizungumza wakati wa hafla ya kumtambulisha mkandarasi huyo (Kampuni ya Giza Cable Industries S.A.E) kutoka Misri ambaye anatekeleza Mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 379 vya mkoa wa Dodoma; Mhe. Senyamule alisema ni muhimu Wananchi kuwekeza mapema katika miundombinu ya ndani ya majengo yao ili kuepuka kuchelewa kupata huduma hiyo.
Mkuu huyo wa mkoa alitoa rai kwa mkandarasi huyo kuhakikisha kazi hiyo ya kusambaza umeme katika vitongoji 379 inakamilika sawa sawa na mkataba au ikiwezekana kabla ya muda uliopangwa.
Aidha, Mkuu wa mkoa Senyamule alionya vikali dhidi ya vishoka; wanaopita kwa Wananchi wa maeneo mbalimba ya mkoa huo akisema kuwa Serikali ya mkoa imejipanga ili kuhakikisha jambo hilo halitokei tena na kutoa wito kwa Wananchi wanawatumia mafundi wenye ujuzi na wanaotambulika kisheria katika kufanya ‘wiring’ ya umeme kwenye nyumba zao.
Kwa upande wake; Mhandisi Msimamizi wa Miradi ya REA Kanda ya Kati, Aneth Malingumu alisema hafla hiyo imelenga kumtambulisha rasmi mkandarasi ili aanze kazi ya kusambaza umeme katika vitongoji vya mkoa wa Dodoma ambapo Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 43.9 kwa ajili ya Mradi huo wa kusambaza umeme kwenye vitongoji 379 katika wilaya ya Chamwino; Kongwa; Mpwapwa; Kondoa na Chemba.
Alisema mradi huo utawezesha Wateja wa awali (Wananchi 12,256) kupata huduma ya umeme na kuongeza kuwa huduma ya umeme ikitumiwa vizuri, itasaidia kuinua uchumi wao pamoja na kuboresha utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo afya na elimu.
Mhandisi Malingumu aliwahimiza Wananchi kuhakikisha wanafanya ‘wiring’ ya ndani ya nyumba mapema ili wawe tayari kuunganishwa na umeme mara miundombinu itakapokamilika na aliongeza kuwa REA itaendelea kushirikiana na mkandarasi ili kutatua changamoto katika maeneo ya kazi na kumlipa kwa wakati ili mradi ukamilike ndani ya muda wa mkataba wa miaka mitatu.
Naye Meneja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, Mhandisi, Donasia Shamba, alisema TANESCO ambaye ndiye Mtaalam Elekezi (Consultant) watahakikisha vifaa pamoja ujenzi wa Mradi huo unazingatia ubora unahitajika ili malengo ya Serikali kupitia REA yafanikiwe.
Kwa upande wake, Mhandisi, Almas Msuya; Mwakilishi wa kampuni ya Giza Cable alisema kampuni hiyo iko tayari kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa na Serikali ili kuhakikisha mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 379 unakamilika kwa wakati kulingana na masharti ya mkataba.



.jpeg)

.jpeg)
.jpeg)

Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...