Hemed Ali, ambaye amehukumiwa hukumu ya kifo katika Mahakama ya Hakimu
Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam leo Oktoba 17, 2022 baada ya kupatikana na hatia ya mauwaji ya, Falihan Maluni, akisindikizwa na Askari Magereza kuingia
katika Chumba cha Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kabla ya hukumu hiyo kutolewa.

Na Karama Kenyunko Michuzi TV
KIJANA Hemed Ally, aliyekuwa akidaiwa kumuua mkata tiketi Farihani Maluni na kumzika nje ya nyumba aliyokuwa amepanga huko Ilala Sharifu Shamba, amehukumiwa kunyongwa hadi kufa baada ya kukutwa na hatia dhidi ya mauaji hayo yaliyotokea 2015

Hukumu hiyo imesomwa leo Oktoba 17, 2022 na Hakimu Mkazi Mkuu Joyce Minde katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya Mahakama kuridhika na ushahidi uliotolewa na mashahidi 12 wa upande wa Jamuhuri pamoja na vielelezo.

Vielelelezo vilivyowasilishwa mahakamani hapo ni pamoja na hati ya amri iliyotolewa ya kufukua mwili huo.

Akisoma hukumu hiyo, Minde amesema pamoja na kwamba ushahidi uliotolewa umeegemea ushahidi wa kimazingira, lakini Mahakama imeweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka kuwa Ally alikuwa na nia ya kuua kwa sababu ya kushindwa kununua gari aina ya Fusso, baada ya marehemu kumpa Sh milioni 30.

Amesema, kwa ushahidi wa mazingira Mahakama lazima ijiridhishe kwa asilimia mia moja bila kuacha shaka lolote kuwa ni kweli kilichotokea ndiyo uhalisia na katika hili mahakama imejiridhisha kuwa mshitakiwa alikuwa ana nia ovu.

Ameongeza kuwa katika ushahidi wao upande wa Jamuhuri wameweza kuthibitisha kuwa kilichofukuliwa Februari 9,2015 eneo la Sharifu shamba, Ilala jijini Dar es Salaam kilikuwa ni mabaki ya mwili wa binadamu na pia kupitia daktari bingwa wa magonjwa ya binadamu na vifo vya mashaka, Innocent Mosha waliweza pia kuthibitisha hilo kwani daktari alidai marehemu Maluni kabla ya kuuwawa na kufukiwa alifungwa kamba ya katani mikononi huku kichwani alifungwa plasta.

"Uthibitisho wa masalia ya Maluni ulithibitishwa kutoka kwenye nguo za marehemu zilizopatikana zikiwa kwenye mabaki hayo ambazo zilithibitishwa na mke wake Tatu Ally ambae alidai ndiyo nguo alizomuandalia mume wake asubuhi ya siku aliyotoweka nyumbani.

Akichambua utetezi wa mshtakiwa Ally, Hakimu Minde amesema upande wa utetezi ulishindwa kumuhoji vizuri shahidi Gumbo kutokana na utetezi wake kuwa alikuja kutoa ushahidi dhidi yake kwa sababu alimfukuza kazi katika kampuni yao pia mshtakiwa hakuweza kuleta mahakamani ushahidi kuwa alihama kwenye nyumba aliyopanga Sharifi shamba kwa sababu ya maji na umeme kuunganishwa kinyume cha sheria.


"Mshtakiwa katika utetezi wake pia alidai mateso na vipigo ndiyo vilimfanya asaini maelezo ambayo hakuyasema yeye, lakini mahakama ilipitia ushahidi na kuona maneno ya maelezo ya onyo na aliyoyatoa mahakamani yanafana


kwa sababu alichokuwa akiuulizwa mahakamani ndicho kilichokuwepo kwenye maelezo ya onyo ikiwemo idadi ya ndugu zake na jina la baba yake mzazi.


Hata hivyo, baada ya hakimu kutamka adhabu ya kunyongwa dhidi ya mshtakiwa, mawakili wa upande wa utetezi ukiongozwa na wakili , Caroline Kigembe hawakusema lolote kuhusu kukata rufaa dhidi ya hukumu hiyo ya kifo.


Awali, Dk Mosha katika ushahidi wake alidai kuwa haikuwa rahisi kujua chanzo cha kifo cha Maluni, lakini kutokana na uwepo wa plasta eneo la fuvu alihisi aliuwawa kwa kuzibwa mdomo na kumsababishia akose pumzi.


Inadaiwa Juni mwaka 2014 Hemed Ally anatuhumiwa kumuua Farihani Maluni eneo la Sharif Shamba ndani ya Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam na kumzika mbele ya nyumba aliyokuwa akiishi.


Mke wa Marehemu, Falihan Malun, wa kwanza kulia, akilia kwa huzuni
baada ya mtuhumiwa wa mauwaji ya mume wako, Hemed Ali, kuhumiwa hukumu
ya kifo baada ya kupatikana na hatia katika Mahakama ya Hakimu Mkazi
Kisutu jijini Dar es Salaam leo Oktoba 17, 2022.

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...