Na MWANDISHI WETU

HALMASHAURI ya Wilaya ya Kisarawe, mkoani Pwani,  imeunda kamati  maalumu itakayo saidia kukuza sekta ya uwekezaji  ikiwa ni hatua ya kuongeza mapato kupitia sekta hiyo.

Kamati hiyo inayoundwa na watu sita  imetangazwa leo katika Mkutano wa Robo ya Kwanza  ya Mwaka  wa Baraza la Madiwani la Halmashauri hiyo.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, Aidan Kitare, ameitaka kamati hiyo kufanya kazi kwa weredi, kuhakikisha  Kisarawe inapaa katika sekta ya uwekezaji , kuinua mapato  na kubuni vyanzo vipya vya  ukusanyaji mapato hayo.

Kitare amesema,  kutokana na usimamizi imara  wa vyanzo vya mapato  halmashauri hiyo inazidi kukua kwa kasi katika ukusanyaji ambapo ndani ya mwezi mmoja tu imekusanya zaidi ya sh. milioni 700 kutoka vyanzo vyake mbalimbali. 

Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, Nyahori Mahumbwe, amesema kamati hiyo itaongozwa na mwenyekiti wake Wakili Alkard Machumu,  ambaye pia ni Ofisa Ardhi wa halmashauri hiyo na Katibu atakuwa Joakim  Costa ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Uwekezaji Idara ya  Maendeleo Biashara Viwanda wa halmashauri hiyo. 

"Dar es Salaam sasa imejaa fursa  za uwekezaji zipo  mkoani   Pwani.  Hivyo tunalazimika sasa kupokea wawekezaji wengi wanaotaka kuwekeza hapa Kisarawe. Tunajiandaa kupokea wawekezaji hao  kwa  kuunda kamati  hii  ya uwekezaji,"amesema Mahumbwe. 

Amesema kamati hiyo  inawajibu wa kuandaa maeneo  muhimu ya uwekezaji ambayo  wawekezaji wanaweza kuwekeza bila kupata changamoto.

"Kwa mantiki hiyo kama kuna maeneo ya uwekezaji  basi yanahusisha ardhi.  Ardhi iwe imepimwa na kuthaminiwa. Tuhakikishe maeneo hayo hayana utata kwa wawekezaji. Ni aibu  mwekezaji anawekeza kisha mwananchi anamshtaki mwekezaji,"amesema.

Amebainisha baada ya uundwaji wa kamati hiyo, kitaundwa kituo cha pamoja 'One Stop Centre'  ya Kisarawe  kurahisisha uwekezaji.

Amesema kituo hicho  kitahusisha  watalaamu wote  kutoka  taasisi zinazoguswa na masuala yanayo hususu  uwekezaji.

 Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati hiyo  Wakili Machumu, amesema  kamati yake  itajikita kuangazia fursa za uwekezaji katika viwanda, utalii, hoteli, kilimo, ufugaji, michezo, burudani na elimu. 

" Pia  tutaanzisha Media kwa maana ya  kituo cha  radio na runinga. Wenzetu  halmashauri nyingi wameanzisha  na wamefika mbali,"amesema.

Amesma kamati imejiandaa kutembelea maeneo yote muhimu katika kata zote za wilaya ya Kisarawe kubaini fursa zilizopo.

"Uwekezaji mwingine ni katika maeneo kando ya misitu  ambako tutajikita katika  uwekezaji wa hoteli  za kitalii, ujenzi wa ukumbi  wa kisasa wa mikutano  kituo cha mabasi .










Na Victor Masangu,Kibaha

Mwenyekiti wa Jumuiya ya  wanawake (UWT) Wilaya ya  Kibaha mjini Elina Mgonja katika kuunga mkono juhudi  za Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan katika kuwakomboa kiuchumi ameamua kutoa darasa la mafunzo ya ujasiriamali.

Akizumgumza katika ziara maalumu ambayo ameifanya kwa wanawake wa UWT  katika kata mbili za Kongowe na Kibaha ikiwa  ni  utekelezaji wa ahadi yake ambayo ameitoa  ya kuwapa ujuzi na mafunzo ya kutengeneza bidhaa mbali mbali.

Mgonja amebainisha kwamba ameamua kutoa mafunzo kwa lengo la kuwapatia ujuzi wanawake hao ambao utawasaidia kwa kiasi kikubwa kuweza kujiajiri na kupambana na wimbi la umasikini.

",Nimeamua kutimiza  kujitolea kuwafundisha Wanawake wa UWT jinsi  ya kutengeneza Sabuni,Vitenge vya Batiki,mafuta ya aina mbalimbali na mambo mengine ya kijasiriamali kwakuwa nataka kuona kila mwanamke anatumia fursa kupitia mafunzo waliyoyapata."amebainisha  Mgonja.

Mgonja amesema kwamba amelenga kufanya ziara hiyo maalumu kwa ajili ya kutoa darasa la ujasiriamali katika kata zote 14 zilizopo ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha.

Mgonja amewaomba Wanawake wa UWT Kibaha Mjini kuhakikisha wanajitokeza kushiriki katika fursa mbalimbali zinazotolewa hususani za kijasiriamali ili waweze kupata elimu  ambayo itawasaidia katika kuondokana na kuwa tegemezi.

"Mimi kama mwenyekiti wenu wa UWT nipo katika ziara yangu kwa ajili ya kufanya mafunzo na darasa maalumu la ujasiriamali na leo tumefanya somo katika kata ya Kongowe na Kata ya Kibaha,"amebainisha Mwenyekiti

Katibu wa UWT Wilaya ya Kibaha Mjini Cesilia Ndaru amewahimiza  Wanawake wa kujitokeza kwa wingi  kushiriki darasa la  mafunzo hayo kwa kuwa yanatolewa bure bila malipo  ya aina  yoyote

Ndaru amesema kipindi hiki ni kipindi cha kufanyakazi na hakuna uchaguzi wowote na kwamba kama kuna mtu anawaza uchaguzi ni wazi kuwa anajipotezea muda ambapo amewaomba Wanawake kuungana na Mwenyekiti katika mafunzo hayo ya ujasiriamali.

Nao baadhi ya wanawake kutoka kata za Kongowe na Kata ya mkuza wamemshukuru Mwenyekiti wa UWT Kibaha mjini kwa kuwawezesha mafunzo hayo ya ujasiriamali ambayo yatawawezesha kujikwamua kiuchumi.

Ziara ya  Mwenyekiti wa jumuiya ya wanawake ( UWT) Wilaya ya  Kibaha Mjini yenye lengo la kutoa mafunzo ya ujasiriamali  yamefanyika katika kata mbili za Kongowe na Kibaha.








Wananchi wenye amana katika benki iliyowekwa chini ya ufilisi ya FBME wamehimizwa kujitokeza kuchukua fedha zao baada ya kubainika kuwa zaidi ya Sh bilioni 2.9 za fidia zinazolindwa na Bima ya Amana bado hazijachukuliwa na wamiliki wake. 

Wito huo umetolewa na Meneja wa Fedha na Uhasibu wa Bodi ya Bima ya Amana (DIB), Romuli Mtui, alipozungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Nanenane Kitaifa yanayoendelea jijini Dodoma Agosti 6, 2026.

Mtui amesema wateja ambao hawajachukua fidia ya kiwango kinacholindwa na Bima ya Amana wanapaswa kufika katika matawi ya Benki ya Biashara ya TCB ili kulipwa, huku wale waliolipwa sehemu ya fedha zao lakini bado wanadai salio la amana zao wakiendelea kufuatilia madai yao katika ofisi za Bodi ya Bima ya Amana zilizopo ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) jijini Dar es Salaam na Dodoma. 

Aidha, amesema malipo ya fidia kwa wateja waliokuwa na amana katika Benki ya FBME upande wa Tanzania tayari yameanza, hivyo wameelekezwa kufuatilia madai yao kupitia ofisi za bodi hiyo au mawasiliano yaliyotolewa kwenye tovuti yake.

Ameongeza kuwa tangu mwaka 2000 jumla ya benki tisa zimewekwa chini ya ufilisi nchini, huku benki saba zilizowekwa chini ya ufilisi mwaka 2017 na 2018 zikiendelea na zoezi la ufilisi ambazo ni  Benki ya Wananchi Mbinga, Benki ya Wananchi Njombe, Benki ya Wakulima Kagera, EFATA Community Bank na FBME Bank, akisisitiza kuwa wateja wote ambao bado hawajachukua fedha zao wanapaswa kujitokeza ili walipwe stahiki zao.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa DIB, Lwaga Mwambande, amesema kila mteja anayefungua akaunti katika benki yenye leseni ya BoT hunufaika na kinga ya amana bila kuchangia moja kwa moja, kwa kuwa michango ya Mfuko wa Bima ya Amana hulipwa na benki wanachama. 

Amesema kiwango cha juu cha fidia kinacholipwa kwa sasa ni Sh milioni 7.5 kwa kila mwekaji endapo benki itafutiwa leseni na kushindwa kuendelea na shughuli zake.

Mwambande amefafanua kuwa wateja wenye amana zinazozidi kiwango hicho hawapotezi fedha zao moja kwa moja, kwani baada ya benki kufungwa huanza mchakato wa ufilisi ambapo mali za benki hukusanywa na kugawiwa kwa wadai kwa mujibu wa sheria, benki zote zinazopokea amana kutoka kwa wananchi huchangia asilimia 0.15 ya amana zao kwa mwaka katika Mfuko wa Bima ya Amana ili kuimarisha uwezo wa kulipa fidia kwa waweka amana.

Amesema pamoja na jukumu la kulipa fidia na kuendesha ufilisi wa benki zilizofungwa, Bodi ya Bima ya Amana pia ina wajibu wa kupunguza hasara kwa kusaidia benki zinazokumbwa na changamoto za kifedha kabla hazijafungwa kupitia utoaji wa mtaji, dhamana au mikopo, hatua inayolenga kuimarisha uthabiti wa sekta ya fedha nchini.





Na Janeth Raphael - MichuziTv 

Serikali imewataka wanawake nchini kuwa waangalifu wanapochukua mikopo, ikisisitiza waepuke mikopo yenye masharti yanayoweza kusababisha migogoro ya kifamilia, kuvunjika kwa ndoa au kupoteza mali zao. Badala yake, imewahimiza kutumia elimu wanayopewa kuchagua mikopo yenye tija itakayowasaidia kukuza biashara na kujikwamua kiuchumi.

Wito huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Amon Mpanju, wakati akifungua Jukwaa la Tatu la Wanawake wa Ushirika Taifa 2026, lililowakutanisha wanawake kutoka vyama mbalimbali vya ushirika kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kiuchumi na uongozi.

Katika hafla hiyo, Dkt. Mpanju pia alizindua Mwongozo wa Jukwaa la Wanawake wa Ushirika Taifa, akieleza kuwa utakuwa nyenzo muhimu ya kuwaongoza wanawake katika uendeshaji wa shughuli zao za ushirika, kuimarisha ushiriki wao katika maamuzi na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za ushirika na wadau mbalimbali kuhakikisha wanawake wanapata mazingira bora ya kushiriki katika shughuli za uzalishaji, ujasiriamali na maendeleo, huku akisisitiza kuwa uwezeshaji wa wanawake ni msingi wa kujenga uchumi imara wa taifa.

Akizungumza katika jukwaa hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirikisho la Vyama vya Ushirika Tanzania (TFC), Farres Muganda, amewataka wanawake wanaoshiriki katika vyama vya ushirika kuongeza uelewa kuhusu masoko, matumizi ya teknolojia na usimamizi wa shughuli za kiuchumi ili kuongeza tija na ushindani.

Muganda amesema wanawake wanahitaji kupata taarifa sahihi kuhusu fursa za masoko na kuendelea kujifunza ili waweze kutumia ipasavyo teknolojia katika uzalishaji na biashara zao. Alieleza kuwa TFC itaendelea kuimarisha jukwaa hilo ili liwe kitovu cha kuwajengea wanawake uwezo wa kushiriki kikamilifu katika maendeleo kupitia mfumo wa ushirika.

Ameongeza kuwa wanawake pamoja na vijana wanapaswa kupewa nafasi zaidi katika shughuli za ushirika kwani makundi hayo yana mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa familia na taifa kwa ujumla.

Aidha, Muganda amesema pamoja na uwepo wa majukwaa zaidi ya 15,000 ya wanawake nchini, bado changamoto ya upatikanaji wa mitaji na mikopo yenye masharti nafuu inaendelea kuathiri ukuaji wa shughuli zao za kiuchumi.

Amewataka wanawake kutumia elimu wanayoipata kupitia majukwaa hayo kufanya maamuzi sahihi ya kifedha, kusimamia shughuli zao kwa ufanisi, kuzingatia sheria na kanuni za ushirika na kutumia fursa za masoko pamoja na teknolojia ili kujenga ushirika wenye tija na kuboresha maisha yao.








Wakulima zaidi ya 1,500 mkoani Morogoro wamenufaika na huduma za kifedha kidijitali zinazotolewa na Mixx by Yas, kupitia malipo ya stakabadhi za ghala pamoja na mikopo nafuu inayopatikana kupitia jukwaa hilo.

Akizungumza katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika mkoa wa Morogoro, Meneja wa Biashara wa Mixx by Yas Kanda ya Pwani Kaskazini, Bw. Anwar Kisesa, alisema huduma hiyo imewanufaisha wakulima wa mazao mbalimbali yakiwemo ufuta, korosho, mbaazi na kakao, na kuwawezesha kupokea malipo yao kwa njia salama, ya haraka na rahisi.

Alisema kampuni hiyo inaendelea kushirikiana na wadau wa sekta ya kilimo ili kuhakikisha wakulima wengi zaidi wanapata huduma za kifedha zitakazorahisisha shughuli zao na kuchangia ukuaji wa uchumi wa vijijini.

Aidha, Bw. Kisesa aliwahamasisha wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nanenane kwa mkoa wa Morogoro kutumia huduma ya Mixx Super App kununua tiketi za kuingia viwanjani pamoja na tiketi za maegesho ya magari, akibainisha kuwa huduma hiyo inasaidia kuepuka foleni na kurahisisha kuingia katika viwanja vya maonesho.
Meneja wa Biashara wa Mixx by Yas Kanda ya Pwani Kaskazini, Bw. Anwar Kisesa,


-Msimu mpya kuanza Oktoba ukitanguliwa na Vodacom Coastal Classic

-Ni mashindano ya mbio za baiskeli za km 109 kutoka Dar hadi Bagamoyo

Katika hatua muhimu kwa maendeleo ya mchezo wa kuendesha baiskeli nchini Tanzania, Vodacom Tanzania Plc kwa kushirikiana na Chama cha Baiskeli Tanzania (CHABATA), leo imetangaza rasmi kubadilishwa kwa jina la msafara wa baiskeli wa Twende Butiama na kuwa Nyerere Cycling Tour, huku pia wakitangaza kuzindua mashindano mapya ya mbio za baiskeli za kilomita 109 za Vodacom Coastal Classic, zinazolenga kuiweka Tanzania kwenye ramani ya kimataifa ya mashindano ya baiskeli.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2016, msafara huu umekuwa ukienzi urithi wa kudumu wa Mwalimu Julius K. Nyerere kwa kuendeleza fursa sawa kwa wote kupitia uboreshaji wa mazingira ya kujifunzia, ujenzi wa miundombinu ya vyoo, pamoja na kuchangia vifaa vya kuwawezesha wanafunzi wenye mahitaji maalum ili kila mtoto aweze kupata fursa ya elimu.

Hadi sasa, msafara huo umefikia zaidi ya shule 107 na kuboresha maisha ya wanafunzi zaidi ya 75,000 wanaofaidika kupitia ujenzi wa madarasa bora na jumuishi yanayokidhi mahitaji ya wanafunzi wote.

Vodacom Tanzania Foundation ilianza kushirikiana na CHABATA kufadhili msafara huu miaka mine iliyopita, na katika kipindi hicho msafara wa Twende Butiama umekuwa mara nne zaidi, huku ukivutia washiriki kutoka Tanzania, ukanda wa Afrika Mashariki na kimataifa. Msafara wa mwaka huu utafanyika kuanzia tarehe 5 hadi 14 Oktoba 2026, washiriki wakianzia Bagamoyo hadi Butiama.

Ili kuakisi dhamira kuu ya msafara huu unaoenzi urithi wa Mwalimu Nyerere huku ndani yake wakipanga kuyawezesha kukua ili kuwa mashindano ya kimataifa ya baiskeli, kuanzia mwaka huu msafara huu utajulikana rasmi kama Nyerere Cycling Tour.

Dhamira ya mwaka huu ni moja: kukuza mchezo wa baiskeli na kuiweka Tanzania katika ramani ya kimataifa ya mchezo wa baiskeli. Kwa kushirikiana na CHABATA, Vodacom Tanzania inazindua mashindano makubwa ya baiskeli ya Vodacom Coastal Classic, yakihusisha mbio za kilomita 109 zitakazoshirikisha waendesha baiskeli wa kiume na wa kike.

Mbio hizi zitaanzia Dar es Salaam, kuelekea kaskazini hadi Makurunge mkoani Pwani na kumalizikia katika eneo la kihistoria la Old Boma, Bagamoyo, zikikamilisha safari ya kilomita 109. Kwa mara ya kwanza mashindano haya yatafanyika Jumapili, tarehe 4 Oktoba 2026, siku moja kabla ya kuanza kwa msafara wa baiskeli wa Nyerere Cycling Tour. Baada ya hapo, Vodacom Tanzania itaendesha mashindano haya kila mwaka ifikapo Jumapili ya kwanza ya mwezi Oktoba.

Kwa mara ya kwanza, washiriki zaidi ya 400 kutoka Tanzania na mataifa mbalimbali duniani wanatarajiwa kushiriki katika mbio hizi, "Tunataka kukuza mchezo huu," alisema Nguvu Kamando, Mkurugenzi wa Vodacom Business. "Kila siku tunaona waendesha baiskeli kwenye barabara zetu, aidha wakiwa ni wataalamu au washiriki wa kawaida. Hakuna sababu kwa nini Abella kutoka Mwanza asiweze kushindana hapa Tanzania na kwenye majukwaa ya kimataifa, au Saidi kutoka Shinyanga. Wanachohitaji ni vifaa sahihi na mafunzo sahihi. Vodacom Coastal Classic inalenga kuhamasisha na kuwapa motisha Watanzania wengi zaidi kuingia katika mchezo huu."

Gabriel Landa, Mwanzilishi wa Nyerere Cycling Tour, alisema, "Nyerere Cycling Tour imekuwa zaidi ya msafara wa baiskeli. Ni kuhusu kuendeleza maono ya Mwalimu Nyerere ya heshima na fursa sawa kwa kila Mtanzania. Kubadilisha jina la mashindano haya kwa heshima yake, sambamba na kuanzisha mbio za kiwango cha kimataifa za Vodacom Coastal Classic, ni mwanzo wa safari mpya. Tunajenga jukwaa ambalo vipaji vya Watanzania vinaweza kuibuka na kuvutia waendesha baiskeli kutoka kote duniani kuja kushiriki.

Tarehe Muhimu

- Vodacom Coastal Classic (Mashindano ya kilomita 109): Jumapili, 4 Oktoba 2026 — Dar es Salaam hadi Makurunge, zikimalizikia Old Boma, Bagamoyo.

- Nyerere Cycling Tour: Tarehe 5–14 Oktoba 2026 — Bagamoyo hadi Butiama.

Kuhusu Nyerere Cycling Tour

Awali ikijulikana kama msafara wa baiskeli wa Twende Butiama, Nyerere Cycling Tour inaenzi urithi wa Mwalimu Julius K. Nyerere kwa kuhamasisha uboreshaji na upatikanaji sawa wa elimu hapa nchini. Kupitia mashindano haya, zaidi ya shule 107 zimewezeshwa na zaidi ya wanafunzi 75,000 sasa wanafaidi mazingira bora na jumuishi ya kujifunzia.

Mkurugenzi wa Vodacom Business Nguvu Kamando,  akizungumza na waandishi wa habari kuhusu msimu mpya wa msafara wa Nyerere Cycling Tour (zamani Twende Butiama) utakaozinduliwa mnamo mwezi wa kumi ukiambatana na mashindano ya mbio za Vodacom Coastal Classic.
Wadau na Washiriki wa msafara wa mbio  za Nyerere Cycling Tour (zamani Twende Butiama) wakipiga makofi kama ishara ya kufurahia ujio wa mashindano ya mbio za Vodacom Coastal Classic.
Wadau wa msafara wa Cycling tour (zamani Twende Butiama) wakisikiliza kwa makini kuhusu msimu mpya wa msafara huo na ujio wa Mashindano ya Vodacom Coastal Classic utakaozinduliwa mnamo mwezi wa kumi mwaka huu.

Mwanzilishi wa Msafara wa Mbio za Twende Butiama, Gabriel Landa  akizungumza na waandishi wa habari kuhusu msimu mpya wa msafara wa Nyerere Cycling Tour (zamani Twende Butiama) utakaozinduliwa mnamo mwezi wa kumi.




Na Mwandishi Wetu, Dodoma
MSULUHISHI wa Migogoro ya Bima (TIO) amewataka wakulima waliokata bima za kilimo kupitia benki au mawakala wa bima, kutumia Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima pale wanapokumbana na migogoro ya fidia ili kupata haki zao badala ya kukimbilia mahakamani.

Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo ya Kimataifa Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samwel Malecela jijini Dodoma, Msuluhishi Mkuu wa TIO Aloyce Mbunito, alisema ofisi hiyo iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria Sura ya 394 ina jukumu la kutatua migogoro ya bima kwa njia mbadala ya mahakama.

Alisema ofisi hiyo pia inalenga kulinda watumiaji wa huduma za bima na kuongeza imani ya wananchi katika sekta hiyo.
Mbunito alisema migogoro inayopokelewa mara nyingi inahusisha kukataliwa kwa madai ya fidia, kulipwa fidia isiyolingana na hasara halisi, kucheleweshwa kwa majibu ya madai pamoja na kutokuelewana kuhusu tafsiri ya mikataba ya bima.

Alisema tangu ofisi hiyo ianze kazi mwaka 2025, imefanikiwa kutatua zaidi ya migogoro 2,015, jambo alilosema linaonyesha kuwa wananchi wameanza kutambua umuhimu wa kuitumia kupata haki zao wanapokumbana na changamoto katika huduma za bima.

Aidha, Mbunito alisema katika maonesho hayo wamepokea viongozi wa vyama vya ushirika vya wakulima kutoka mkoani Mara, waliowasilisha changamoto zinazowakabili wakulima wa tumbaku waliopata hasara kutokana na mvua ya mawe, licha ya kuwa walikuwa wamekata bima kupitia benki.

Kwa mujibu wa Mbunito, changamoto kubwa iliyobainika ni baadhi ya wakulima kutofahamu kampuni za bima zilizowahudumia kwa kuwa walikata bima kupitia benki zilizokuwa mawakala wa kampuni hizo.

Alisema pia baadhi ya wakulima hawana mikataba ya bima, ambayo ni nyaraka muhimu katika kufuatilia madai ya fidia pale wanapopata hasara.

Naye Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Mara (WAMACU), Momanyi Range, alisema elimu waliyoipata katika banda la Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima imewafungua macho kuhusu umuhimu wa kuwa na mikataba ya bima pamoja na kuhifadhi ushahidi wa majanga.

Alisema ushahidi huo unaweza kujumuisha picha za mazao yaliyoharibiwa na majanga, hatua ambayo inaweza kusaidia kurahisisha mchakato wa madai ya fidia.

Range alisema chama hicho sasa kitawaongoza wakulima walioathiriwa kukusanya malalamiko yao, kupata mikataba ya bima kutoka benki husika na kuyawasilisha katika Ofisi ya Msuluhishi wa Migogoro ya Bima ili kuhakikisha wanapata haki zao.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuwawezesha wakulima kukabiliana na hasara zinazotokana na majanga na kuendelea na shughuli za uzalishaji bila kuathiriwa zaidi na athari za majanga hayo.

Dodoma
RAIS wa Chama cha Mawakili wa Serikali Tanzania, Wakili Boniventure Mwambaja, amesema anaiona Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kuwa ni miongoni mwa taasisi bora za maendeleo ya miundombinu barani Afrika kutokana na mafanikio makubwa yaliyopatikana tangu kuanzishwa kwake mwaka 2017.

Wakili Mwambaja ametoa kauli hiyo alipotembelea banda la TARURA katika Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nanenane yanayofanyika Kitaifa katika uwanja wa Dkt. John Malecela mkoani Dodoma.

Akizungumza baada ya kupata maelezo kuhusu shughuli na mafanikio ya wakala huo, amesema TARURA imeonyesha maendeleo makubwa katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi na matengenezo ya barabara za vijijini na mijini hatua ambayo imechangia kuboresha huduma za usafiri na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

"Ni dhahiri kuwa TARURA imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa majukumu yake ya ujenzi na matengenezo ya barabara tangu kuanzishwa kwake. Vilevile, imefanikiwa kuwajengea uwezo watumishi wake wanaosimamia miradi mbalimbali jambo linalodhihirishwa na mrejesho chanya kutoka kwa wananchi", amesema Wakili Mwambaja.

Ameongeza kuwa ongezeko la mtandao wa barabara zinazopitika katika maeneo mbalimbali nchini pamoja na utatuzi wa haraka wa changamoto katika maeneo korofi ni ushahidi wa dhamira na ufanisi wa wakala huo katika kuwahudumia wananchi.

TARURA inaendelea kushiriki Maonesho ya Kilimo ya Nanenane yenye kauli mbiu "Tambua Soko; Ongeza Tija kutekeleza Dira 2050" kwa kutoa elimu kuhusu majukumu yake, mafanikio yaliyofikiwa na huduma mbalimbali zinazolenga kuboresha miundombinu ya barabara za vijijini na mijini nchini.
 


Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Wilaya ya Kinondoni, Saad Mtambule ameipongeza shule ya Green Acres ya jijini Dar es Salaam kwa kuwa ya kwanza kuanzisha klabu ya Uhamiaji.

Alitoa pongezi hizo akiwa shuleni hapo wakati akizindua klabu hiyo ambapo aliambatana na Afisa Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam, Vicent Haule na Meya wa Kinondoni, Songoro Mnyonge.

Mtambule alisema Wilaya yake inashule Zaidi ya 200 hivyo watapita shule baada ya shule kushawishi kuhakikisha kila shule inakuwa na klabu ya uhamiaji kama moja ya mbinu ya kuwafanya watoto wakatae uhamiaji haramu tangu wakiwa wadogo.

“Tutapita kuhamasisha shule zianzishe utaratibu huo ili wanafunzi wote wajue masuala ya uhamiaji wakiwa wadogo, tunapenda wahamiaji lakini wanaofuata taratibu na sharia za nchi yetu kwa hiyo lazima tuwajenge watoto kuchukua wahamiaji haramu tangu huku chini,” alisema

“Hata mama nyumbani anapotengeneza keki anatengeneza ili watoto wake wale sasa wakija watoto wa jirani wakila ile keki watoto wako wakakosa haipendezi, lazima tuwatolee taarifa kwa viongozi watu tunaoona kwamba ukaazi wao hapa nchini unamashaka mashaka,” alisema

Alisema Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Ubungo itaibeba ajenda ya uhamiaji kama moja ya masuala nyeti kuhakikisha hakuna mtu anayeingia nchini na kukaa bila kufuata utaratibu kwenye wilaya hiyo.

“Kuna watu wanarubuniwa na vitu vidogo vidogo ili wawafiche hawa wahamiaji haramu, natoa wito tusithubutu kuwapa nafasi wahmiaji haramu kukaaa kwenye maeneo yetu kwasababu tukikubain umemficha tukamkamata nawewe utakakatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria,” alisema

DC alilishukuru Jeshi la Uhamiaji nchini chini ya Dk Anna Makakala kwa namna ambavyo limefanikiwa kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha linadhibiti wawhamiaji haramu.

Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Songoro Mnyonge alisema kuanzishwa kwa klabu hiyo ni mafanikio makubwa sana kwani wanafunzi watakuwa na uwezo wa kufahamu madhara ya wahamiaji haramu tangu wakiwa wadogo.

“Nimuhimu sana kurithisha vijana hawa wadogo umuhimu wa kukataaa wahamiaji haramu kwasababu madhara yake yanajulikana, kuanzishwa kwa klabu hizi ni moja ya mambo ya msingi kabisa ya kupigiwa mfano,” alisema

“Nawapongeza Green Acres kwa uamuzi wa kukubali klabu hii kuzinduliwa hapa shuleni mmekuwa wa kwanza Mkoa wa Dar es Salaam, na kwa bahati nzuri shule hii iliasisiwa na mheshimiwa diwani wetu wa Magomeni Bujugo ambaye ametangulia mbele za haki lakini maono yake bado yanaishi,” alisema

Aidha, Meya Songoro alimpongeza Mkurugenzi wa shule ya Green Acres, Jackline Rushaigo kwa namna ambavyo amemudu kusimamia na kuendeleza maono ya baba yake kwa kuifanya shule hiyo kuendelea kuongoza kitaaluma.

Naye Mkurugenzi wa shule hiyo, Jackiline Rushaigo alilishukuru Jeshi la Uhamiani nchini kwa kuichagua shule hiyo kuwa ya kwanza kuanzisha klabu hiyo miongoni mwa maelfu ya shule zilizoko nchini.

“Mmeona namna tunavyolea vipaji vya wanafunzi wetu, tunajitahidi kuwalea kwenye maadili mem asana hata wanapokuwa nje ya shule wanakuwa watu wema sana na nawaahidi kuwa klabu hii itakuwa msaada mkubwa sana kwa taifa letu,” alisema

Alisema wameamua kuanzisha klabu hiyo hapo shuleni kama sehemu ya kuwajengea uzalendo wa kuipenda nchi yao na kukataa kuona watu wasio raia wakiishi nchini bila kufuata taratibu na sheria za nchi.





 
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda, ameshangazwa na kiwango cha ubunifu wa teknolojia zinazobuniwa na kuzalishwa na kampuni ya Mati Technologies baada ya kutembelea banda la kampuni hiyo katika Maonesho ya 33 ya Kitaifa ya Kilimo (Nane Nane 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma.

Mhe. Pinda alitembelea banda hilo leo na kupokea maelezo kutoka kwa viongozi na wataalamu wa Mati Technologies kuhusu shughuli mbalimbali zinazofanywa na kampuni hiyo katika kubuni na kutengeneza teknolojia zinazolenga kuongeza tija katika sekta ya kilimo na maeneo mengine ya maendeleo.

Katika ziara hiyo, alikagua teknolojia mbalimbali zinazotengenezwa na kampuni hiyo, ikiwemo ndege nyuki zinazotumika kunyunyiza viuatilifu na mbolea mashambani kwa usahihi, haraka na ufanisi mkubwa, pamoja na mifumo mingine ya kisasa ya kiteknolojia inayolenga kuboresha uzalishaji wa kilimo.

Baada ya kushuhudia namna teknolojia hizo zinavyofanya kazi, Mhe. Pinda alisema ameridhishwa na hatua kubwa ya ubunifu iliyofikiwa na wataalamu wa Kitanzania.



“Ni jambo la kujivunia kuona Watanzania wakibuni na kuzalisha teknolojia za kisasa zinazotoa suluhisho kwa changamoto mbalimbali za maendeleo, hususan katika sekta ya kilimo,” alisema.

Alisema maendeleo hayo yanaonesha uwezo mkubwa wa wataalamu wa ndani katika kubuni teknolojia zinazokidhi mahitaji ya nchi na kuchangia kukuza uchumi kupitia sekta ya kilimo na viwanda.


Aidha, aliipongeza Mati Technologies kwa kuwekeza katika utafiti, ubunifu na uzalishaji wa teknolojia za ndani, akisisitiza kuwa juhudi hizo zinapaswa kuungwa mkono ili kuharakisha maendeleo ya taifa na kuongeza ushindani wa bidhaa za Kitanzania katika soko la ndani na kimataifa.

Kwa upande wake, uongozi wa Mati Technologies ulisema kampuni itaendelea kubuni na kuzalisha teknolojia zenye ubora wa hali ya juu zitakazorahisisha shughuli za uzalishaji, kuongeza tija kwa wakulima na kuchochea matumizi ya teknolojia katika sekta mbalimbali za uchumi.





Maonesho ya Nane Nane yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuonesha mafanikio ya sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda na teknolojia, huku yakivutia maelfu ya wananchi, wakulima, wawekezaji, wanafunzi na wataalamu kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Kupitia ubunifu wa teknolojia zinazozalishwa hapa nchini, Mati Technologies inaendelea kujijengea sifa kama moja ya kampuni zinazochochea matumizi ya sayansi, teknolojia na utafiti katika kuongeza tija ya uzalishaji na kuchangia maendeleo endelevu ya Tanzania.